Wednesday, February 18, 2015

Rais wa TFF, Jamal Malinzi ana changamoto kubwa ya kuinua soka la Bongo

Na Oswald Ngonyani

PENGINE inaweza ikawa ni kauli ambayo itaonekana kuwaghadhabisha wengi, lakini acha tu niuweke wazi ukweli huu, kwani nikikaa kimya nitakuwa miongoni mwa watu wasioitakia mema nchi hii hasa katika tasnia ya mchezo wa soka.

Soka la bongo ni la kijanjajanja, kila mdau wa soka analijua hilo kinagaubaga. Viongozi wa soka la bongo ni wajanjajanja, wachezaji nao ni wajanjajanja pia. Hata mashabiki nao wana hulka hizo hizo za ujanja ujanja.

Hakuna ustahimilivu wa soka hapa Tanzania. Ubabe, Vitisho na hata Chuki ni nguzo zilizo wazi zinazoonekana kuongoza soka la bongo. Hakuna dalili ya kufika tunakokutarajia, tutafikaje huko tunakokutaka wakati marubani wetu ni wajeuri?

Hakuna ‘seriousness’. Hakuna uzalendo tena, watendaji wakuu wenye dhamana ya kuiongoza soka yetu wapo kama hawapo huku wakiwa vibaraka wakubwa wa maswahiba wao wanaoongozwa na hulka ya ujeuri, kiburi pamoja na fitna, vitu ambavyo havikutakiwa kupewa nafasi lakini wao wamevipa nafasi.

Nakumbuka Msimu uliopita (2014) kulijitokeza madudu mengi sana katika soka letu watanzania na hata kuleta hali ya sintofahamu miongoni mwetu sisi kwa sisi. Ubovu huu wa kiutendaji unawahusu viongozi wote, yaani viongozi wa juu soka wa letu mpaka wa chini katika ngazi ya vilabu.

Kuna mambo makubwa ambayo Viongozi wetu katika ngazi ya juu waliyafanyia kazi kimizaha sana na hata kutoa majibu marahisi mno, majibu ambayo kwa kiasi kikubwa yaliwafanya wadau wengi wawaone viongozi hao kama wana nia ya kudidimiza soka la Tanzania, badala ya kuboresha.

Dkt. Damas Ndumbaro amefungiwa miaka saba

Pengine walikuwa sahihi lakini kwa bahati mbaya jamii ya wafuasi wa soka la bongo hawakuwaelewa. Wakati fulani suala la kufungiwa miaka saba kwa daktari wa sheria, Dk. Damas Ndumbaro lilionekana kuibua mjadala mzito sana ambao mpaka leo upo japo makali yake yamepungua.

Yaliyotokea kuhusu sakata hilo ni mengi, na hata kuwafanya mashabiki na wafuasi wa soka la bongo wabakie katika pande mbili zinazokinzana. Wapo walioiunga mkono TFF kwa maamuzi yake hayo lakini pia wapo waliokuwa upande wa Ndumbaro ambao unaonekana kuwa na watu wengi zaidi.

Sarakasi za namna hii si ngeni katika soka la bongo, ni vitu ambavyo vipo na vinatokea mara kwa mara tena kwa namna ya pekee sana hutangazwa sana katika Vyombo vyetu vya Habari na hata kuwafikia watanzania walio wengi.

Yapo mengi sana ambayo viongozi wetu wanayafanya na hata kuwapa hasira mashabiki wa soka la bongo. Mbali na viongozi hao wa ngazi ya juu, vilabu vyetu navyo vinafanya madudu mengi ambayo yanawafanya mashabiki wao wabaki babaikoni.

Hii yote inachagizwa na ujanja ujanja wa Viongozi lakini pia wachezaji wa timu husika. Leo hii mchezaji mkongwe katika soka la bongo Shaaban Kisiga ‘Marlon’ ametoweka katika kambi ya timu yake ya Simba mara baada ya mchezo dhidi ya Mbeya City. Huo ni utovu wa nidhamu lakini pia ni hulka ile ile ya ujanja ujanja.

Juma Nyosso amefungiwa mechi 8 kwa utovu wa nidhamu

Tangu alipoondoka, awali viongozi wa timu husika walionekana kudai kuwa mchezaji huyo alipewa ruhusa maalumu lakini baadaye yeye mwenyewe Kisiga alitanabaisha kuwa ameondoka bila ruhusa na kamwe hatarudi tena klabuni hapo.

Kuna kitu nimejifunza hapo kuhusu suala hili. Si mchezaji pekee hata Viongozi wake wote kwa pamoja wanaangukia katika nadharia hii ya ujanja ujanja, Kiongozi anasema hili, lakini mchezaji na yeye anakuja na kuzungumza lake, hii ndiyo taswira halisi ya soka la bongo.

Sahau kuhusu sakata la Juma Nyosso wa Mbeya City kuhusu kumpapasa makalio mshambuliaji wa Simba Elias Maguri na baadaye kuamua kuomba msamaha. Sahau kuhusu sakata la Tambwe na yule beki wa Ruvu Shooting.

Lakini pia fanya kumbukizi kuhusu ishu ya Emmanuel Okwi aliyepigwa kiwiko na beki wa Azam FC. Kwa neno rahisi sana, matukio yote haya yaliyofanywa na wahusika yanaendana na hulka zile zile za ujanja ujanja.

Misimu kadhaa iliyopita Mshambuliaji machachari wa Yanga alikuwa akiitumikia klabu ya Simba na hata alipomaliza mkataba wake aliamua kwa dhati ya moyo wake kuchukua mamilioni ya Simba kwa lengo la kusaini mkataba mpya kwa klabu hiyo, lakini baadaye akaamua kusaini Yanga. Maisha ya mwanandinga huyo kwa sasa yanasikitisha sana.

Ujanja ujanja aliokuwa ameufanya kwa kuchukua pesa katika pande mbili zinazokinzana yaani Simba na Yanga leo hii zinamjutisha kijana huyu aliyewahi kuwazimia simu maafisa fulani wa timu kutoka nje ya nchi waliokuja bongo kuisaka saini yake eti ili wakimpigia wasimpate.

Nakumbuka wakati fulani Uongozi wa Klabu ya Yanga ulifunguka kuwa hauhusiki na deni la mshambuliaji wao huyo anayedaiwa fedha na Benki ya CRDB kwa kuwa yeye aliomba udhamini katika timu hiyo na si kulipiwa kama anavyodai.

Ngassa alinukuliwa akidai kushindwa kuwa katika kiwango kizuri cha kuitumikia timu yake hiyo kufuatia deni la shilingi milioni 45 alizokopa CRDB kwa ajili ya kuilipa Simba ili ajiunge na Yanga, baada ya kusaini timu mbili kwa madai kuwa uongozi wa timu hiyo ungemsaidia laki tano kila mwezi jambo ambalo Yanga wamelipinga.

Ujanja ujanja wake aliokuwa ameufanya sasa unamfanya akose amani ya moyo wake. Mbwembwe zote za pale TFF wakati ule alipoenda kulipa deni la Simba sasa hazipo tena. Wale waliomsindikiza kwa bashasha nyingi wamejiweka kando pasi kumpa msaada wowote. Ujanja ujanja wake umemponza.

Kuna mengi sana ya kuandika kuhusu minajili ya soka la bongo kwa sasa, soka ambalo kwayo limetawaliwa na hulka ya ujanja ujanja miongoni mwa mioyo ya tuliowapa dhamana ya kutuongoza lakini pia wachezaji wetu nao wana hulka ile ile, hulka ambayo kamwe haitatufikisha kokote. Hulka ya ujanja ujanja.

Tubadilike sasa. Naam ni wakati muafaka sasa kwa viongozi wa soka nchini kubadilika. Mabadiliko haya yaanzie juu lakini pia yaje mpaka kwenye vilabu ambapo Viongozi wa timu pamoja na wachezaji wao watatakiwa kuwajibika kwa kadri inavyopasika na siyo kuendekeza hulka ya ujanja ujanja.

TUKUBALI KUWA TUMEANGUKA, TUINUKE, TUANZE SAFARI UPYA YENYE KULETA TIJA KWA SOKA LA BONGO.


Unapenda kuwa Mkufunzi wa mchezo wa soka? Nunua sasa Kitabu cha ‘SIRI YA SOKA’ Uweze kuwa na uelewa zaidi katika mchezo huo, Wasiliana na Mwandishi wa Makala haya kwa  simu namba 0767 57 32 87 ili kuweza kujipatia nakala ya Kitabu hicho.

0 comments:

 
https://www.sexmutant.com/ https://www.sexindrag.com/ porn movies sex videos hd porno video