Yanga wameshaanza mazoezi chini ya kocha mkuu, Mbrazil Marcio Maximo
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
0712461976
Imechapishwa Julai 3, 2014, saa 2:39 asubuhi
MSIMU wa 2014/2015 wa ligi kuu soka Tanzania bara unatarajia
kuanza kutimua vumbi mwezi agosti mwaka huu ambapo timu 14 zitachuana vikali kusaka
taji linalomikiliwa na mabingwa Azam fc.
Ili kujiimarisha kwa ajili ya changamoto ya msimu
mpya mpya, timu kadhaa zimeshaanza maandalizi ya kabla ya msimu `pre-sesson`
wakiwemo Azam fc na Yanga sc.
Kama ilivyo kawaida, timu kubwa zimeshaanza mawindo,
lakini baadhi ya timu zimelala usingizi wa `pono` mpaka sasa zikisubiri wiki
mbili kabla ya ligi kuanza.
Maandilizi ya aina hii yanaitwa `zima moto`. Watu
wa zima moto huwa wanakuwa na presha kubwa pale mambo yanapoanza kushika kasi.
Kwa hali ya kawaida, sio rahisi kufanikiwa kutwaa ubingwa kwa kufanya
maandalizi ya wiki mbili au tatu.
Unakumbuka msimu wa mwaka 2012/2013 Yanga
walilazimika kuweka kambi ya wiki mbili nchini Uturuki na kufanikiwa kutwaa
ubingwa. Msimu wa 2013/2014 walirudi tena Uturuki kwa maandilizi ya mzunguko wa pili na ligi ya
mabingwa.
Kwa kiasi kikubwa Yanga walifanikiwa, japokuwa
huwezi kusema mambo ya Uturuki pekee ndio yaliwafanye wawe na makali dhidi ya
Al Ahly, katika mechi mbili za ligi ya mabinga zilizopigwa Dar es salaam na Alexndria
nchini Misri.

Watatetea ubingwa?: Azam fc ndio mabingwa watetezi wa ligi kuu, hivyo msimu ujao wana kibarua cha kulisaka taji hilo kwa mara ya pili pamoja na kuiwakilisha nchi katika michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika.
Ikumbukwe katika safari ya Azam fc, msimu wa 2012/2013 wao walienda
kuweka kambi nchini Afrika kusini. Lakini msimu uliofuata hawakuweka kambi nje
ya nchi, lakini waliendelea kujifua vikali katika uwanja wao wa kisasa wa Azam
Complex uliopo Mbande, nje kidogo ya jiji la Dar es salaam. Maandilizi hayo
yaliwafanya wafanikiwe kuwa mabingwa msimu wa 2013/2014.
Na kwa muda mrefu sasa wapo kambini kujiwinda na
msimu mpya na tayari uongozi unasubiri kocha mkuu, Mcameroon, Joseph Marius
Omog aweke wazi programu yake ya kambi ya nje ya nchi.
Meneja wa Azam, Jamedari Said alisema jana kuwa
uongozi unamsikiliza Omog na popote anapotaka kwenda kuweka kambi watamfanikishia
safari na mambo yote ya kambi.
Huu ni ueledi wa uongozi wa Azam kwani wanatambua
soka sio uchawi, bali ni maandalizi tu. Pia wanatambua mwakani wana kibarua cha
ligi ya mabingwa baranI Afrika ambapo watakutana na miamba ya soka.
Wakati Azam fc ambao ni mabingwa watetezi wakiwa
katika maandalizi, makamu bingwa Dar Young Africans, tayari nao wameshaanza
mazoezi katika fukwe za koko beach na uwanja wa Bandari Tandika jijini Dar es
salaam.

Msimu ujao nani ataibuka kidume baina ya Logarusic wa Simba sc na Maximo wa Yanga?
Yanga wamekuja na nguvu mpya baada ya kumuajiri
kocha Mbrazil, Marcio Maximo. Huyu ni kocha anayeufahamu utamaduni wa Tanzania
kwani aliishi kutoka mwaka 2006 mpaka 2010 akiifundisha timu ya Taifa ya
Tanzania, Taifa Stars.
Mbeya City fc walishika nafasi ya tatu msimu
uliopita baada ya kukusanya pointi 49 katika mechi 26 walizocheza.
Ukiwa msimu wao wa kwanza, nafasi hiyo haikuwa
mbaya kwao, lakini bila shaka wana mipango ya kuendeleza mafanikio hayo msimu
ujao.
Mbeya City fc ni moja ya timu iliyochangia ligi
kuu kuwa maarufu msimu uliopita. Kila kona ilikuwa gumzo na kila mpenda michezo
alitamani kuona timu nyingine kama hii zinakuja ligi kuu.
Kwasasa wanasikika wakisema wamesitisha usajili
kwasababu wachezaji waliopo wanatosha. Mbeya City bado hawajaanza programu rasmi
ya mazoezi, ingawa wanaendelea kujifua
mdogo mdogo.
Simba walioshika nafasi ya nne kwa kujikusanyia
pointi 38 wao wametoka katika hekaheka za uchaguzi, hivyo haijawa rahisi kwao
kuanza maandalizi kama ilivyo kwa wapinzani wake Yanga, Azam fc na Mbeya City.
Evans Eliaza Aveva amechaguliwa kuwa rais wa
kwanza wa klabu hiyo. Huyu ni moja ya watu wa `Friends of Simba`. Hili ni kundi
lenye nguvu zaidi katika klabu hiyo.

Watamzuia Mnyama tena?: Simba walimaliza nafasi ya nne nyuma ya Mbeya City nafasi ya tatu. Logarusic na bosi wake Aveva watakubali msimu ujao?
Ushindi wake unatafsiriwa kurejesha nguvu ya
mamilionea hawa wa Friends of Simba ( F.O.S) mitaa ya Msimbazi. Aveva alimwaga
sera safi kabisa ikiwemo kufanya usajili wa nguvu ili kuirejesha klabu hiyo
kwenye soka la ushindani.
Sasa yametimia na alishinda kwa kishindi, watu
wanasubiri usajili wa haraka ili waanze maandalizi chini ya kocha wao mkuu,
Mcroatia, Dravko Logarusic.
Uzuri ni kwamba mwenyekiti wa kamati ya usajili ya
Simba, Zacharia Hans Poppe alisema tayari wameshafikia mazungumzo na wachezaji
wanaowahitaji, lakini alikataa kuwapa mikataba mpaka watakapopatikana viongozi
wapya. Zoezi hilo limekamilika na bila shaka majina yataanza kuanikwa na kuona
picha za wachezaji wakisaini mikataba mipya, japokuwa kuna wameshafanya kwa
mmoja
Ukiziangalia timu zilizoshika nafasi nne za juu,
Azam fc, Yanga, Mbeya City na Simba sc. Unaona zina nia ya kuendeleza mafanikio
ya msimu uliopita au kuzidisha zaidi.
Azam watakuwa na kibarua cha kutetea ubingwa,
Yanga watakuwa na kibarua cha kurejesha taji jangwani, Mbeya City fc watakuwa na
kibarua cha kusaka ubingwa, Simba watakuwa na kibarua cha kurudisha heshima kwa
kutwaa ubingwa.
Kutokana na mazingira haya, ni rahisi kusikia timu
hizi zikianza maandalizi mapema.
Ruvu Shooting walishika nafasi ya sita kwa
kujikusanyia pointi 38 nyuma ya Kagera Sugar.
Klabu hii inayonolewa na kocha Mkenya Tom Alex
Olaba ilishaanza maandalizi ya msimu mpya na umekamilisha usajili wa wachezaji
watano wapya. Shooting inaonekana kujipanga na kuwa na nidhamu ya mpira.
Maandilizi ni muhimu katika mchezo wa soka.
Lakini kuna timu ambazo hazikufanya vizuri
kutokana na uzoefu wao, lakini zimekaa kimya. Labda zinafanya mambo kimya
kimya, lakini sidhani kama zipo katika maandalizi `bab kubwa`.

Mtakuja na jipya?: Simba hii haikufanya vizuri msimu uliopita.
Wapi Kagera Sugar, Mtibwa Sugar, Tanzania Prisons,
Coastal Union, Mgambo JKT?. Binafsi nilitegemea kusikia maandalizi ya nguvu kwa
timu hizi kutoka na matokeo ya `kuungaunga` waliyopata msimu uliopita, lakini
imekuwa tofauti.
Yawezekana baadhi ya timu hizo zina tatizo la uchumi,
lakini nyingine sidhani kama zina tatizo hilo. Kinachoonekana ni kukosa
mipango.
Timu nyingi zina malengo ya kushiriki ligi kuu na
si kushindana. Malengo yao yanakuwa kubaki ligi kuu tu, lakini mambo mengine kama
kusaka ubingwa hawana muda kufikiria.
Ili kupata ligi bora zaidi ya msimu uliopita,
ingekuwa bora kwa timu zote kuanza maandalizi ya mapema. Nasikia habari za
Ndanda fc, Stand United na Polisi Morogoro.
Hizi ni timu mpya. Naambiwa zimeshaanza maandalizi
na zinazionya timu zilikuwepo msimu uliopita. Sina hakika zitakuja kwa kasi
ipi, lakini naamini zimejipanga vizuri.
Viongozi wa timu za ligi kuu maandalizi ya mapema
ni mazuri sana. Kuna njia nyingi za kuiandaa timu hata kama huna hela.
Kumbuka kufanya vizuri kunaleta udhamini. Hamuoni
milioni 360 za Bin Slum katika klabu ya Mbeya City fc?, ni matunda ya kufanya
vizuri.
Hata kama hamna hela ya kutosha kuweka kambi,
tumieni utaratibu wa wachezaji kutoka majumbani kwao na kufanya mazoezi ya
nguvu pamoja.
Sibezi maandalizi ya timu yoyote, lakini nakumbusha
kuwa kila jambo linaanza na maandilizi bora.
Kila la heri timu za ligi kuu soka Tanzania bara kuelekea
msimu mpya wa wa 2014/2015 unaotarajia kuanza kushika kasi mwezi agosti mwaka
huu.

0 comments:
Post a Comment