
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
Imechapishwa Julai 3, 2014, saa 2:09 asubuhi
WASHINDI wa tatu wa ligi kuu Tanzania bara msimu
uliopita, Mbeya City fc wamesitisha suala la usajili wa wachezaj kwa ajili ya
msimu mpya wa ligi kuu unaotarajia kuanza mwezi Agosti mwaka huu.
Katibu mkuu wa klabu hiyo, Emmanuel Kimbe amesema
wamefanikiwa kusajili wachezaji watatu tu kama alivyoelekeza kocha mkuu, Juma
Mwambusi.
“Kikubwa ni kwamba, sisi katika suala la usajili,
hatujasajili wachezaji wengi sana. Tumesajili wachezaji watatu tu na tumemaliza
usajili kwa upande wetu. Katika idadi hiyo ya wachezaji, yupo Them Felix kutoka
Kagera Sugar”. Alisema Kimbe.
Kimbe aliongeza kuwa wachezaji hao watatu
wanatosha na sasa wanaelekeza nguvu kubwa katika timu yao ya pili itakayosaidia
kujenga timu ya wakubwa.
“Tumefanya kwa mahitaji kwasasa. Wachezaji wetu
wengi wapo, kwahiyo hatukuona sababu ya kujaza wachezaji ambao hatutawatumia.
Kwanza unawakosea, unawatumia chini ya asimilimia 10, si jambo zuri”.

“Tuna wachezaji wanaoweza kutumika vizuri kwa
mujibu wa mahitaji ya mwalimu. Kwa nafasi alizopendekeza, tumefanyia kazi, na
maeneo mengine yapo vziuri”. Aliongeza Kimbe.
Hata hivyo Kimbe aliwataka wapenzi wa Mbeya City
fc kutulia kwasababu wana mkakati mzito wa kufanya mabadiliko ndani ya klabu.
Alifafanua kuwa wapo watu mikataba yao
imeshamalizika, huku wengine wakiongezewa na wengine hawataongezewa.
“Kila kitu tunachofanya ni kuifanya klabu kuwa ya
kisasa. Kuna mabadiliko ya kiuongozi, benchi la ufundi na wachezaji, lengo ni
zuri tu”. Alieleza Kimbe.
Siku chache zilizopita, aliyekuwa kocha msaidizi
wa klabu hiyo, Maka Mwalwisyi alitangaza kuachana na klabu hiyo baada ya
mkataba wake kumalizika mwezi mei mwaka huu.
Maka alieleza kuwa aliamua kuachana na Mbeya city
fc ili kupata changamoto mpya hasa baada ya kupata kozi ya leseni B ya CAF
iliyofanyika jijini Dar es salaam.
Kocha huyo muumini wa soka la vijana alisema sasa
anahitaji kupata timu ya kuwa kocha mkuu ili aitambulishe falsafa yake tofauti
na alipokuwa anafanya kazi chini ya falsafa ya bosi wake, Juma Mwambusi.

0 comments:
Post a Comment