0712461976
Imechapishwa Julai 9, 2014 saa 3:53 asubuhi
LUIZ Felipe Scolari amekubali kubeba lawama zote
kutokana na fedheha waliyoipata Brazil kutoka kwa `watu katili` Ujerumani.
Haikutegemewa na wengi kama Brazil wangeingia
katika rekodi mbaya ya kombe la dunia kwa kufungwa mabao 7-1 na Ujerumani
katika mchezo wa nusu fainali ya kombe la dunia jana usiku.
Brazil waliojiamini, waliingia kwa kasi, lakini
bao la mapema la Thomas Muller liliwatoa upepo ghafla ya kufungisha mabao mengi
zaidi.
Bora Neymar hakuwepo katika mchezo huo. Huyu ni
mchezaji mwenye kiwango cha juu kama alivyo kwa Lionel Messi na Cristiano
Ronaldo.
Kama angekuwepo uwanjani, halafu Brazil ikafungwa
mabao kama ya jana, basi ingemharibu zaidi katika maisha yake ya soka.
Tatizo kubwa la Brazil lilikuwa kwenye safu ya
ulinzi iliyoongozwa na nahodha David Luiz, Maicon, Marcelo na Dante. Hawa
walikuwa tatizo jana, walikaba vibaya, utulivu ulikuwa `F`. Hata Neymar
angekuwepo, kwa aina ya uchezaji wake, bado safari ya Brazil ingefika mwisho
kwasababu asingekuwa na jinsi ya kuwaokoa.

Mambo ya `wedi kapu` haya, si mchezo: David Luiz alishindwa kuzuia machozi baada ya `mbungi` kumalizika.
Pole sana Scolari, pole sana Neymar, Pole sana
Thiago Silva, pole sana wananchi wa Brazil, pole sana mashabiki wa Brazil
duniani kote. Huo ndio mpira wa miguu, Rekodi yenu itazungumzwa zaidi ya miaka
50 ijayo.
Hongereni Ujerumani kwa ushindi mnono. Hongereni
kwa Miroslav Klose kuvunja rekodi ya gwiji wa Brazil, Ronaldo. Mabao 16 na kuwa
mfalme wa mabao wa kombe la dunia ni heshima kubwa.
Kwa umri wa miaka 36, kwa watu wengine wangeona hustahili
kuingia kikosi cha Ujerumani kilichosheheni nyota wengi. Lakini kwa kutambua
umuhimu wa rekodi, mlimchukua ili atimize malengo yake. Klose ameheshimiwa na
kupewa nafasi, na mwisho kafikia malengo. Hongera Mkongwe.

Jukwaani nako kulikuwa na majanga, Mjerumani `Katili` sana
Dunia ilisimama kwa dakika 90 jana, shughuli
zilisimama kushuhudia nini kimewakumba mabingwa hao mara tano wa dunia.
Wakati kocha Scolari akiumiza kichwa jana, kwa
upande wa makocha wa Simba sc, mambo yanatakiwa kuendelea kama kawaida.
Kocha msaidizi wa Simba, Seleman Abdallah Matola
anatarajia kuanza kuiongoza klabu hiyo katika mazoezi ya kujiandaa na msimu
mpya wa ligi kuu kuanzia leo julai 19, 2014 kwenye uwanja wa Boko Veteran uliopo
Boko.
Matola ataanza majukumu hayo wakati huu ambao kocha
mkuu wa klabu hiyo, Mcroatia Dravko Logarusic hajawasili nchini.
Kwa taarifa za ndani ya Simba sc, Loga anaweza
kuwasili kesho alhamisi na ijumaa
kujiunga na Matola kuendeleza gurudumu la maandalizi.
Huu ni wakati mwingine muhimu kwa Simba.
Wanahitaji kuwaunga mkono makocha wao, wachezaji wao ili waiendeleze klabu hii.
Kwa miaka mitatu sasa, Simba imekuwa akiwaumiza
mashabiki wake. Matokeo yake yamekuwa ya kuungaunga tu, hivyo kuna ulazima kwa
kila mwanasimba kutoa mchango wake kwa nafasi aliyonayo.

Kocha Mkuu wa Simba sc, Mcroatia, Dravko Logarusic (wa kwanza kushoto) ana kazi ya kuijenga klabu hiyo.
Makocha kazi yao ni kufundisha mbinu za uwanjani,ufundi
wa kucheza mpira, kuwajenga wachezaji
kisaikolojia na mengine ya kitaalam. Ili kufanya kazi hii lazima uwe na taaluma.
Loga na Matola wana nafasi ya kukaa na wachezaji
kwa muda mwingi kuliko mtu yeyote. Wao ndio wanajua nani mzuri nani mbaya. Wao
wanajua nidhamu ya mchezaji mmoja mmoja.
Kwa kifupi, masuala yote ya kitaalam ya uwanjani,
wao ndio mabosi. Hapa hakuna wa kuingilia, kama ikitokea mtu wa nje na benchi
la ufundi kaingilia, ujue ndio siasa za Simba na Yanga hizo, pamoja na timu za
majeshi.
Cha msingi, makocha waachwe wafanye kazi kwa
kuzingatia ueledi wao. Anachoweza kufanya mtu wa nje, ni kushauri tu, tena sio
lazima ushauri uchukuliwe.
Benchi kama sehemu ya kwanza ya timu, liachwe
lifanye kazi yake ili malengo ya kuijenga timu yatimie. Wanasimba, waungeni
mkono Loga na Matola ili wawarudishe katika hadhi yenu.

Sehemu nyingine muhimu katika kuijenga Simba sc,
ni wachezaji wenyewe.
Wanandinga wa Simba lazima mjue kuwa kuna watu
wengi nyuma yenu. Fanyeni kazi yenu kwa bidii. Nidhamu ni kitu cha msingi.
Maandalizi mazuri yatawapa matokeo mazuri.
Zingatieni maelekezo ya makocha na kuongezea akili
zenu.Hamuwezi kufundishwa kila kitu, jifunzeni mbinu mpya ili muisaidia Simba.
Mchango wa viongozi chini ya Rais, Evans Aveva, ni
kusaidia mambo ya kiutawala. Wao wana wajibu wa kuhakikisha mambo yote ya
kambi, mazoezi, mishahara,posho na mengine yanayohitaji fedha yanafanyika kwa
wakati.
Watanzania tunajijua maisha yetu. Bila kupewa
kichache cha mfukoni, kazi inalala, na hii inatokana na kutegemewa zaidi pale
unapokuwa na hela.
Baadhi ya wachezaji wanasomesha, wana familia,
wanategemewa na watu tofauti tofauti, hivyo kuwacheleweshea posho na mishahara,
unawaondolea ufanisi wa kazi.

Big Bosi: Rais wa Simba sc, Evans Elieza Aveva
Aveva jukumu lako ni kumaliza tatizo hilo ambalo
katika uongozi wa Ismail Aden Rage lilionekana kusumbua. Mara kadhaa lawama
ziliibuka na yeye alikiri kwa kinywa chake kuwa kulikuwa na tatizo hilo.
Wachezaji waheshimiwe, wathaminiwe na kupata haki
zao mapema. Hii itaongeza morali katika harakati za kuijenga Simba.
Sina tatizo na mipango yako Aveva, sera zako
zilikuwa nzuri. Wanachama walikuamini na kukupa kura nyingi. Sasa muda wa
utekelezaji uanzie hapa kwenye mazoezi.
Nimeambiwa utakiweka kikosi kambini nchini Afrika kusini, tena kwa
siku 17 kuanzia julai 20. Nadhani ni wazo zuri ambalo litawapa wachezaji
utulivu mkubwa.

Kwa upande wa wanachama na mashabiki, kazi yenu ni
moja tu. Ni kuunga mkono juhudi hizo na kusubiri ligi ianze ili muishangilie
timu yenu. Mna haki ya kutoa maoni kwa viongozi wenu na benchi la ufundi,
lakini sio lazima yachukuliwe. Ndio maana ya maoni.
Msiwape presha wachezaji na makocha wenu. Mkifanya
mambo kwa utulivu na kumuacha kila mtu atekeleze majukumu yake basi itakuwa
jambo jema.
Simba sc, kumekucha, agosti sio mbali. Ligi iko
karibu. Sasa tulizeni akili katika maandalizi.
Kila la Kheri Mnyama Simba kuelekea msimu mpya.
Tunasubiri kuwaona upya ili ladha ya utani wa jadi irudi kama zamani.

0 comments:
Post a Comment