
Kocha mkuu wa Mbeya City fc, Juma Mwambusi (katikati) akiongea na Hassan Mwasapili (kushoto) na Richard Peter (Kulia)
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
0712461976
Imechapishwa Julai 2014, saa 5:37 asubuhi
DUNIA imepandwa na `mzuka bab kubwa` wa kutaka kujua nini timu nyingine ya Amerika (Argentina) itafanya katika mchezo wa leo wa nusu fainali ya pili ya kombe la dunia dhidi ya Uholanzi ya Van Gaal.
Argentina ikiwa na Lionel Messi inatarajiwa kufuta
machozi ya Waamerika baada ya wenyeji Brazil kutandikwa kipigo cha kihistoria
cha mabao 7-1 na Ujerumani.
Wakati kila mtu akiisubiri mechi hiyo kwa hamu, klabu
ya Mbeya City fc iliyoleta ushindani mkubwa wa ligi kuu inatakiwa kufanya mambo
muhimu kwa ajili ya kuendeleza mafanikio yake.
Msimu uliopita Mbeya city chini ya kocha bora wa
Msimu, Juma Mwambusi ilishika nafasi ya tatu kwa kukusanya pointi 49 na kuiacha
Simba katika nafasi ya nne.
Yanga walishika nafasi ya tatu na Azam fc walitwaa
ndoo kwa mara ya kwanza katika historia yake.
Nafasi ya tatu kwa klabu changa kama Mbeya City
yalikuwa mafanikio. Ugeni wa wachezaji katika michuano ya ligi kuu uliathiri
kwa baadhi ya mechi kubwa kama ile dhidi ya Yanga, Simba na Azam fc.
Ligi kuu iligeuka kuwa maarufu zaidi kutokana na
ujio wa Mbeya City fc.
Sasa timu hii inaelekea kucheza msimu wake wa
pili. Miaka ya 80, Tukuyu Stars walipanda ligi kuu na kutwaa ubingwa, lakini
msimu uliofuata walishuka daraja.
Baadhi ya watu wanadiriki kuwatabiria Mbeya City
hali hii. Lakini ni mapema kusema yanaweza kutokea.
Mpaka sasa klabu hii inayomilikiwa na Halmashauri
ya jiji haijaanza mazoezi rasmi. Kwa taarifa zilizopo ni kwamba wanatarajia
kuanza maandalizi julai 15 mwaka huu.
Hawajafanya usajili mkubwa kwasababu sera yao
haiwaelekezi kusajili wachezaji wengi wakongwe, wanajali soka lao la vijana.
Wamemnasa mshambuliaji, Them Felix `Mnyama` kutoka kwa `wanankulukumbi ` Kagera
Sugar.
Juma Mwambusi amebainisha kuwa kwasasa anaangalia
uwezekano wa kusajili viungo wa ukabaji ili kuimarisha kikosi chake.
Mbeya City ni moja ya klabu niliyotarajia iingie
kambini mapema kama walivyofanya Azam fc, na Ruvu Shooting.
Beki wa Mbeya City fc, Hassan Mwasapili akichuana na Erasto Nyoni wa Azam fc msimu uliopita katika dimba la Sokoine.
Kuchelewa kwa kambi kumechangiwa na majukumu ya
kimataifa waliyokuwa nayo. Walienda nchini Sudan kushiriki michuano ya CECAFA Nile
Basin Cup.
Hii ilikuwa changamoto nzuri kwao, na walitolewa
hatua ya robo fainali. Waliporudi, waliamua kuwapa mapumziko wachezaji wao.
Hawakuwa na jinsi na ndio maana mpaka sasa hawapo kambini.
Licha ya hayo, Mbeya City lazima watambue mambo
kadhaa yaliyopo mbele yao yakiwemo yafuatayo:
Mosi; wana kibarua cha kuendeleza mafanikio ya
msimu uliopita. Kuna haja ya kujipanga kwa hili. Moja ya tatizo la timu za
Tanzania ni kushindwa kuendeleza pale walipofikia. Kwa mfano, timu inachukua ubingwa, lakini msimu unaofuata
inakuwa mbovu tena. Hili ni tatizo linalotokana na mipango mibovu ya viongozi
pamoja na kutimua makocha. Leo hii Simba ya akina Okwi haipo tena. Walifanya
mazuri, msimu uliofuata walipoteana.
Mbeya City fc wanatakiwa kujua hili, nafasi ya
tatu yalikuwa mafaniko, lakini wanatakiwa kusonga mbele zaidi. Tunatarajia
kuwoana wakiwa washindani wa ubingwa. Kwa bahati nzuri wamebakiza wachezaji wao
wengi.

Mbeya City walishiriki michuano ya CECAFA Nile Basin nchini Sudan na kuishia hatua ya robo fainali
Ili kuendeleza mafaniko yao, lazima waje na
mipango mingine. Kuna Dravko Logarusic wa Simba ambaye hatakubali kuona Simba
inazingua tena. Kuna Marcio Maximo wa Yanga anayetaka kurejesha ubingwa na kuna
Joseph Marius Omog wa Azam anayetaka kutetea ubingwa.
Mwambusi kazi haitakuwa rahisi kwake, lazima ajiandae
mapema kwa ushindani wa msimu ujao. Nimewataja makocha watatu ambao ni `Levo`
ya Mwambusi. Lakini wapo makocha wengine ambao watampa chanagamoto mfano, Fred
Minziro wa JKT Ruvu, Tom Olaba wa Ruvu Shooting, Jackson Mayanga wa Kagera
Sugar, Mecky Mexime wa Mtibwa Sugar na
wengineo.
Pili; Mbeya City itakuwa na wapinzani wengi kama
ilivyo kwa Simba, Yanga na Azam fc.
Kila timu itakayokwenda Sokoine itakuwa inajipanga
vilivyo. Upinzani utakuwa wa hali ya juu. Kutakuwa na uwezekano wa kukamia
mechi kwasababu Mbeya City iko usawa wa kutafuta ubingwa. Pia mechi za ugenini
zitakuwa na changamoto kubwa kama inavyotokea kwa Simba na Yanga.
Kagera Sugar ikicheza na Ruvu Shooting, kiwango
huwa cha kawaida, lakini ikikutana na Yanga, Simba, mpira unakuwa mgumu sana.
Kwahiyo tutegemee mechi ngumu zitazoikutanisha
Mbeya City fc kwasababu ni timu tishio. Kwa mazingira haya, Juma Mwambusi ana
kazi kubwa ya kuandaa kikosi chake.

Tatu; Baadhi ya wachezaji wa Mbeya City fc
watakuwa wanakabwa kama akina Amisi Tambwe wa Simba sc, Mrisho Ngassa wa Yanga
na Kipre Tchetche wa Azam.
Wachezaji wa timu ndogo huwa wanawakamia wachezaji
hatari wa timu kubwa za Simba, Yanga na Azam fc. Msimu ujao, Mwegane Yeya, Paul
Nonga, Saady Kipanga watakuwa wanaangaliwa
kwa jicho lingine. Lazima watakuwa wanawekewa ulinzi mkali. Pia kumbuka, Them
Felix kaongezeka.
Kwa wachezaji hawa hatari wa Mbeya City,
wanatakiwa kutambua hili na kuanza maandalizi ya mapema ili kutafuta mbinu
mpya.
Nne: Mbeya City fc watambue kuwa watakosa huduma
ya kocha msaidizi, Maka Andrew Mwalwisyi aliyemaliza mkataba wake na kuamua
kuiacha klabu hiyo kwasababu anataka timu ya kuwa kocha mkuu. Hii imetokana na
yeye kuwa na leseni B ya ukocha ya CAF.
Maka ni mwalimu mzuri na mwenye kipaji cha
kuhamasisha na kushauri wachezaji. Anajua kufundisha soka la vijana na anajua namna ya kuishi nao.
Hata wakati akiwa Mbeya City fc, mara kadhaa
nilipata nafasi ya kukaa naye. Na kila tukiwa pamoja kambini, wachezaji
walikuwa wanamtumia kwa mambo mengi ikiwemo kumuomba ushauri.
Kuondoka kwa kocha huyu, ni pigo. Najua wapo
makocha wengi, lakini huwezi kufuta umuhimu wa Maka katika klabu ya Mbeya City
fc.
Kinachotakiwa kwa viongozi wa klabu hii ni kutulia
na kutafuta msaidizi wa aina ya Maka ili amsaidie Mwambusi.
Nguvu ya benchi la ufundi iongezwe. Mwambusi
anatakiwa kupata mshauri na msaidizi wa aina ya Maka. Bila kufanya hivyo, kuna
kitu kitapungua.

Tano; mashabiki wajipange mambo ya `Mtonyo` mfukoni. Msimu uliopita, walisafiri kwa
gharama zao kwenda kuishangilia timu kila ilipokuwa inakwenda kucheza mechi.
Sasa isiwe nguvu ya soda, msimu ujao wanatakiwa kuendeleza moto ule ule.
Ina faida kubwa sana kwa wachezaji kila wanapoona
kuna watu nyuma yao, hakika wanapata morali ya kuucheza mpira kwa ustadi.
Mashabiki wa Mbeya City msirudi nyuma. Kazeni buti
mpaka kieleweke.
Mbeya City fc wadau wanatamani kuwaona katika
kiwango kikubwa zaidi ya msimu ulipoita.

0 comments:
Post a Comment