Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam
YANGA SC na Mbeya City fc zimekutana katika mechi
ya nne ya ligi kuu soka Tanzania bara tangu City wapande msimu uliopita.
Msimu uliopita, Yanga walitoka sare ya 1-1 uwanja
wa Sokoine kabla ya kuwafunga Mbeya City bao 1-0 uwanja wa Taifa Dar es salaam.
Msimu huu mechi ya kwanza kule Mbeya, Yanga
walishinda mabao 3-1 uwanja wa Sokoine na leo wametoa kipigo kama hicho uwanja
wa Taifa.
Mabao ya Yanga yamefungwa na Kpah Sherman, Salum
Telela na Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
Bao la kufutia machozi la Mbeya City limefungwa na
Themi Felix ‘Mnyama’.
Kwa matokeo haya, Yanga wameendelea kuwa wababe
dhidi ya timu inayomilikiwa na halmashauri ya jiji la Mbeya.
Matokeo ya leo yanawafanya Yanga wazidi kupaa
zaidi kileleni wakijikusanyia pointi 46 baada ya kucheza mechi 21.
Nafasi ya pili inashikiliwa na mabingwa watetezi
Azam fc wenye pointi 38 kufuatia kushuka dimbani mara 20 na hapo jana walitoka
sare ya 1-1 dhidi ya Mtibwa Sugar uwanja wa Manungu, Turiani, Mkoani Morogoro.
RIPOTI YA MECHI
Yanga waliandika bao la kwanza dakika ya 8' kupitia kwa Kpah Sherman akimalizia krosi ya Oscar
Joshua na kumzidi ujanja beki Juma Nyosso.
Dakika ya 37' Yanga waliandika
bao la pili kupitia kwa Salum Telela aliyepiga shuti la chini chini akipokea
mpira wa adhabu ulichongwa na Haruna Niyonzima na mpira kuwapita mabeki wa
Mbeya City na kutinga nyavuni.
Dakika mbili baadaye, (dk 39'0) Themi Felix aliifungia goli la kwanza
Mbeya City akipokea pasi ya Kenny Ally na kutulia kisha kuburuza mpira
eneo la hatari na kumtazama kipa Ally Mustapha na kufunga goli zuri kwa ‘kuchipu’.
Dakika chache kabla ya kwenda mapumziko timu nzote
mbili zilishambuliana kwa zamu, lakini mabeki wa timu zote walikuwa makini
kuonoa hatari.
Hadi dakika 45 zinamalizika, Yanga walikuwa mbele
kwa magoli 2-1.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi, Yanga
wakitengeneza nafasi kwa haraka.
Dakika ya 49' Nadir Haroub aliifungia
Yanga goli la tatu kwa kichwa akimalizia mpira wa adhabu uliopigwa na Niyonzima
Dakika ya 53' Mbeya City walipata pigo
kufuatia Them Felix kuoneshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja na Mwamuzi Akrama
baada ya kumchezea vibaya Salum Telela.
Kocha Juma Mwambusi alifanya mabadiliko dakika ya
59' akiwatoa wachezaji wawili ambapo
Deus Kaseke alikwenda benchi nafasi yake ikachukuliwa na Peter Mapunda,
Raphael Alfa naye akaenda benchi nafasi yake ikachukuliwa na Yusuph Abdallah.
Dakika ya 61' Salum Telela alishindwa kuendelea na
mchezo kutokana na madhambi aliyofanyiwa na Themi na nafasi yake ikachukuliwa
na Hassan Dilunga.
Dakika ya 69' Tambwe alipiga kichwa akimalizia
krosi ya Saimon Msuva, lakini mpira ukagonga mwamba wa kushoto kwa
chini.
Dakika ya 70' Yanga walifanya mabadiliko, Sherman
alikwenda benchi na nafasi yake ikachukuliwa na Mrisho Ngassa.
Dakika 10 za mwisho, timu zote zilishambuliana kwa
zamu, lakini hakuna aliyekuwa na hesabu nzuri za kufunga goli.
REKODI ZA MAGOLI YALIYOFUNGWA LEO
Kpah Sherman amefunga goli la pili tangu atue Yanga,
Goli lingine alifunga dhidi ya Coastal Union, Yanga wakishinda 8-0 jumatano ya
wiki hii uwanja wa Taifa.
Salum Telela naye alifunga goli la kwanza msimu
huu dhidi ya Coastal Union na leo amefunga goli la pili dhidi ya Mbeya City.
Bao la Themi Felix ni la tano msimu huu tangu
ajiunge na Yanga kutoka kutoka Kagera Sugar.

0 comments:
Post a Comment