MLINZI wa kati wa Azam fc, Said Hussein
Morad ametangaza kuwa mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake na mabingwa
hao watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara.
Katika mahojiano maalumu na mtandao huu,
Morad amesema mkataba wake umemalizika jana aprili 16 mwaka huu na Azam
hawajaonesha nia ya kumuongezea mkataba mpya.
“Namshkuru Mungu nimeishi na Azam
vizuri, hakuna matatizo yoyote yaliyotokea na hata kama mashabiki wanadhani
kuna matatizo yametokea, kwangu mimi hakuna matatizo na hivi sasa mimi ni
mchezaji huru, amesema Morad na kuongeza: “ Mkataba wangu umeisha na ndio maana
mashabiki wangu hawanioni kwenye timu.
“Mkataba wangu umeisha jana tarehe
16/4/2015. Sijawahi kukaa na viongozi ila taarifa nilifikisha mpaka kwa meneja na
yeye akafikisha mpaka kwa kocha, lakini baada ya hapo hawanielezi chochote”.
Amesema Morad.
VIPI KUHUSU TAARIFA ZA KUFUNGIWA MECHI
4 PAMOJA NA AGGREY MORRIS NA KIPRE TCHETCHE?
Morad amejibu: “Mimi nilikuwa
sijasimamishwa, niliomba ruhusa, katika msiba wa Simba Ukawa kulikuwa na
familia yangu, wale Marehemu mmojawapo ni damu yangu (mjomba wake Rajab Uhadi Mtoro),
Azam walinipa ruksa ya siku mbili, lakini maiti kutoka Morogoro ikachelewa kuja
Muhimbili, ilikuja kama saa 11 alfajiri na kufanya michakato ya pale ilichukua
muda na unajua Muhimbili maiti haiwezi kutoka mpaka kuandikisha jina. Nikawa
nasubiriwa mimi kwasababu ndiye niliyeandikisha jina na baada ya kufika ndipo
michakato ikaanza”.
“Tukaanza kuosha maiti na kusafirisha
mpaka Bagamoyo nyumbani na baadaye tukafikisha kijijini kwetu Kigogo na kuzika”
KURUDI KAMBINI ILIKUWAJE SASA?
Morad anasema: “Siku ya pili ilitakiwa
niripoti kwenye mechi, tulikuwa tunacheza na Mbeya City na mini nikawa njiani kurudi
na nilipofika nikarudi na kwenda moja kwa moja kambini siku ya mechi”.
AKAAMBIWA NINI?
Morad anatiririka: “Baada ya mechi
kuisha, jioni nikaambiwa Morad inabidi
urudi nyumbani mpaka tutakapokwenda Morogoro na Tanga, tukirudi kutoka Tanga
tutakuita, kocha ananiambia kitu kama hicho”
“Baada ya pale nikamwambia kocha mimi
mkataba wangu unaishi mpaka siku hiyo na nitakuwa nimeshamaliza mkataba na Azam”
ILIKUWAJE AKAHUSISHWA NA UTORO WA
KIPRE, MORRIS?
Morad anafafanua: “Aggrey Morris, Kipre
Tchetche walisimamishwa kwa matatizo yao na namimi nikachanganywa,mimi
niliwaomba ruksa, sema baada ya kuwaomba hiyo ruksa nilipoenda kambini nikajumuishwa
kundi la akina Aggrey, lakini mimi sina kosa lolote”
“Hapo kwenye kujumuishwa sijui kwanini
ilikuwa hivyo, ujue kila mtu na maisha yake, kama kocha ana mapungufu yake au
mchezaji nina mapungufu yangu, lazima
uongozi ukae na kuamua”
IMEKUWAJE AMEWAAMBIA AZAM FC KWA MUDA
MREFU KUHUSU KUONGEZA MKATABA LAKINI WAMEMCHUNIA?
Morad anasema: “Naamini hawanihitaji
kwasababu niliwaambia muda mrefu kabla miezi miwili haijaisha”
VIONGOZI WA AZAM WALIMFARIJI MSIBANI?
Morad anasisitiza: “Hakuna hata kiongozi
mmoja wa Azam aliyekuja kwenye msiba wangu isipokuwa wa Simba waliowafuata watu
wao
.Wachezaji walionipigia simu ni Aggrey
na Mwaikimba na Erasto”.
VIPI MIPANGO YAKE?
Morad anasema: “Kama timu yangu ya Azam
itaniongeza mkataba nitafanya kazi kwasababu sina kinyongo na timu yoyote
Tanzania. Kama hawataniongeza nipo tayari kuichezea timu yoyote”.


0 comments:
Post a Comment