
WAGONGA nyundo wa Mbeya, Mbeya City fc wametamba
kuibuka na ushindi dhidi ya Yanga katika mechi ya ligi kuu Tanzania bara itakayopigwa
mwishoni mwa wiki hii uwanja wa CCM Sokoine, Mbeya.
Afisa habari wa klabu hiyo, Dismas Ten amesema
licha ya kuvuna pointi moja mwishoni mwa wiki iliyopita dhidi ya Coastal Union
uwanja wa Mkwakwani kufuatia matokeo ya suluhu, Mbeya City hawako tayari
kupigwa na Yanga.
“Tunajua Yanga wametoka kushinda mabao 2-0 dhidi
ya BDF XI ya Botswana. Ushindi wao umetokana na aina ya wapinzani wao, watambue
wanakuja kucheza na Mbeya City yenye uchu wa kupata matokeo”. Amesema Dismas.
“Mbeya City ni timu bora na miaka michache ijayo
itakuwa timu yenye mashabiki wengi zaidi nchini kuwakaribia Simba na Yanga, ina
mipango mikubwa sana”. Ameongeza tena.

Kwa upande wa Yanga, Mkuu wa Idara ya Habari na
Mawasiliano, Jerry Muro amesema baada ya kuichapa BDF kombe la Shirikisho
wanaelekea Mbeya kuchukua pointi tatu muhimu dhidi ya Mbeya City.
“Tumejiandaa vizuri, hatuna cha kupoteza. Kila mtu
aliona kiwango chetu, nguvu ile tunaipeleka Mbeya mwishoni mwa wiki dhidi ya
Mbeya City, bila wasiwasi wowote tunachukua pointi tatu”. Amesema Muro.
Msimu uliopita katika uwanja wa Sokoine, Mbeya
City ilitoka sare ya 1-1 dhidi ya Yanga na mechi ya marudiano ikapigwa bao 1-0
uwanja wa Taifa Dar es salaam.

0 comments:
Post a Comment