Beki
wa Kushoto wa Maafande wa Jeshi la Kujenga Taifa, Ruvu Shooting Stars,
Stephano Mwasyika (Kulia) akiwa kwenye shughuli yake wakati walipokutana
na Mnyama Simba SC mzunguko wa kwanza wa ligi kuu soka Tanzania bara
mwaka huu
…………………………………………………………………………………………………………………………………
Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
Beki
wa kushoto wa maafande wa Ruvu Shootinga ambaye pia aliwahi kuzichezea
klabu za Prisons, Moro United, na Mabingwa Yanga msimu uliopita,
Stephano Mwasyika amewashauri waamuzi wa ligi kuu soka Tanzania bara
kujenga utamaduni wa kuthamini mawazo ya wachezaji wanapochezesha mechi
mbalimbali.
Mwasyika
amesema waamuzi wengi wa kitanzania hawana uwezo wa kuwasikiliza
wachezaji uwanjani hata kama wamekosea kutafsiri sheria.
“Mwamuzi
anaweza kukosea kitu fulani, mchezaji unamfuata, hataki kukusikiliza.
Soka sio uhasama jamani, sijui hawajifunzi kwa wenzao wa Ulaya, mara
zote wamekuwa wakizungumza na wachezaji kuhusu mambo mbalimbali ya
uwanjani, hasa wanapokosea”. Alisema Mwasyika.
Beki
huyo anayesifika kwa kupiga pasi za uhakika aliongeza kuwa waamuzi ndio
wenye maamuzi ya juu katika mechi, lakini lazima wakubali kuwa wao ni
binadamu, hivyo kukosea ni kawaida.
“Katika
kila kazi, kukosea kupo tu, hakuna ambaye hakosei. Lakini ukikosea na
ukakubali kuwa umekosea, inakuwa nzuri zaidi. Waamuzi lazima
wajifunze.”. Alisema Mwasyika.
Mwasyika alisisitiza kuwa baadhi ya waamuzi kwa kukosa ustaarabu wanadiriki mpaka kutoa matusi ya nguoni.
“Mimi
siwezi kutaja mtu, lakini kwenye mechi moja pale uwanja wa Taifa msimu
huu, kuna mwamuzi mmoja alimtukana mchezaji matusi ambayo siwezi
kuyasema. Nawaomba wajifunze kutoka `Videoni` namna ya kuwasiliana na
wachezaji, na ndio maana kunatokea mambo ya kukunjana na kupigana”.
Alisema Mwasyika.
Hata
hivyo, Mwasyika amewapongeza waamuzi waliochezesha ligi kuu mzunguko wa
kwanza kwa madai kuwa wamejitahidi kufanya kazi yao, lakini wakijifunza
suala la mawasiliano na wachezaji, itawajengea ufanisi katika kazi yao.


0 comments:
Post a Comment