NDANDA FC imelazimika kuongeza utulivu katika kipindi hiki
cha usajili ili kupata wachezaji wataoifanya kuwa timu tishio msimu wa
2015/2016 wa ligi kuu soka Tanzania bara.
Kaimu katibu mkuu wa Ndanda, Seleman Kachele amesema wapo
wachezaji wengi waliopo kwenye rada zao na wanawaangalia kwa jicho la
kitaalamu.
“Wachezaji wapo wengi, sisi hatusajili majina ya wachezaji,
tunasajili kwa kitaalamu na tunaamini tutakuwa na wachezaji wazuri wataoifanya
timu iwe vizuri. Tumekuwa na utulivu, tuko hatua za mwisho mwisho,
tukikamilisha tutawatangazia. Tunaweza kusajili wachezaji wa nje ya Tanzania au
hapa hapa nchini kutegemea na matakwa ya mwalimu”. Amesema Kachele.
Kachele ameweka wazi kwamba ripoti ya mwalimu aliyemaliza
mkataba na klabu hiyo, Meja Mstaafu, Abdul Mingange imebainisha mapungufu
kadhaa yaliyojitokeza msimu uliopita.
“Mingange katika ripoti yake amesema mapungufu yapo kwenye
kikosi, anataka wachezaji wengine kama mabeki wa pembeni, kulia na kushoto,
mabeki wa kati, golikipa na kiungo mchezeshaji”. Amesema Kachele na kuongeza: “
Kocha mpya Jumanne Chale ataangalia hayo na kuongezea yakwake, lakini sisi
hatuwezi kusajili mchezaji wa kimataifa mwenye uwezo sawa na mchezaji wa hapa
mjini”.
0 comments:
Post a Comment