Imechapishwa Agosti 16, 2014, saa 5:34 asubuhi
CRISTIANO Ronaldo ameupinga mjadala unaoendelea
kwasasa kuwa mchezaji mwenzake wa Real Madrid, mlinda mlango, Iker Casillas
zama zake zimepita.
Ronaldo amesisitiza kuwa nahodha huyo wa Hispania
bado yupo katika ‘Kiwango cha dunia’.
Kipa huyo alikabiliwa na misimu miwili migumu
baada ya kupoteza namba mbele ya Diego Lopez na kuonesha kiwango cha chini
katika fainali za kombe la dunia majira ya kiangazi mwaka huu nchini Brazil na
kushuhudia Hispania ikitolewa hatua ya makundi.
Licha ya kiwango chake cha karibuni, kuuzwa kwa
Lopez katika klabu ya AC Milan kunamrejesha Casillas kama kipa namba moja mbele
ya kipa mpya aliyesajiliwa, Keylor Navas.
Ronaldo alisema timu itakuwa katika mikono salama
chini ya kipa huyo mwenye miaka 33 ambaye ameshinda makombe matatu ya UEFA,
mawili ya mashindano ya Ulaya na kombe la dunia.
“Iker hajawahi kutoka katika orodha ya makipa bora
wa dunia,” Ronaldo aliwaambia waandishi. “Siku zote amekuwa katika kiwango cha
dunia”.
Madrid walifungua pazia la UEFA kwa kutwaa kombe
la ‘UEFA Super Cup’ dhidi ya Sevilla, huku Ronaldo akifunga mabao yote mawili
katika ushindi wa 2-0 na Mreno huyo alisisitiza kuwa kombe hilo ni mwanzo tu wa
kutetea ubingwa wa UEFA.
Vijana hao wa Carlo Ancelotti wanaendelea na
maandalizi ya msimu na leo watakuwa na mechi ya kirafiki dhidi ya Fiorentina
kabla ya kuanza mchezo wa ufunguzi wa La liga dhidi ya mahasimu wao, Atletico
Madrid jumanne ijayo.


0 comments:
Post a Comment