Kaimu
 Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Kuhifadhi Wanyamapori Tanzania Bw.John Muya 
akifafanua kwa waandishi wa habari kuhusu mikakati ya mfuko huo 
inayolenga kuongeza mapato yake ikiwemo ujenzi wa jengo 
litakalojulikana  kama kakakuona,kushoto ni Kaimu Katibu Tawala wa mfuko
 huo Bi Antonia Raphael.
1. UTANGLIZI
Mfuko
 wa Kuhifadhi Wanyamapori Tanzania (TWPF) ulianzishwa mwaka 1978 baada 
ya kufanya marekebisho (ammendmend) ya kifungu cha 69 cha Sheria ya 
Kuhifadhi Wanyamapori (Wildlife Conservation Act) Na. 12 ya mwaka 1974. 
Marekebisho hayo yalitangazwa kwenye Gazeti la Serikali Na. 21 la tarehe
 22 Mei, 1981.
Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya sasa Na.5 ya mwaka 2009 inabainisha uwepo wa Mfuko kisheria katika kifungu cha 91(1). 
Mfuko
 ulianzishwa kwa lengo la kuiongezea Idara ya Wanyamapori uwezo wa 
kifedha wa kutekeleza majukumu yake ya ulinzi wa wanyamapori. Serikali 
ilitambua kuwa ulinzi wa wanyamapori unahitaji fedha nyingi na fedha 
kutoka Hazina hazikidhi mahitaji yaliyopo.
Mfuko
 hugharamia majukumu mbalimbali ya Idara ya Wanyamapori ikiwa ni pamoja 
na  uzuiaji ujangili, uendelezaji wa mapori ya akiba, usimamizi wa 
matumizi ya wanyamapori, utunzaji wa kanzidata  na kuwezesha watumishi 
kuhudhuria mafunzo mbalimbali. 
2. UZUIAJI UJANGILI
Mfuko
 hugharamia shughuli za doria ndani na nje ya Mapori ya Akiba na doria 
za kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu ikiwa ni pamoja na 
kukabiliana na tatizo la kunguru weusi katika mikoa mbalimbali nchini.
Mfuko
 hufanya malipo ya kifuta machozi kwa wananchi ambao ndugu zao wameuawa 
au kujeruhiwa na wanyamapori. Aidha, Mfuko hulipa kifuta jasho kwa 
wananchi ambao mashamba yao yameharibiwa na wanyamapori. Wananchi ambao 
mashamba yao yameharibiwa na wanyamapori wanatakiwa kutoa taarifa kwenye
 ofisi ya kijiji iliyopo karibu ndani ya siku tatu tangu uharibifu 
ulipotokea. Uongozi wa kijiji husika hutoa taarifa Wilayani ili wataalam
 wa kilimo na wanyamapori wafanye tathmini ya uharibifu uliotokea. 
Kwa
 upande wa watu wanaojeruhiwa au kuuawa na wanyamapori ni lazima 
uharibifu uthibitishwe na dakatari. Aidha, ni lazima awepo shahidi 
kutoka katika eneo husika ambaye si ndugu wa familia iliyoathirika ili 
kuepuka udanganyifu. Uongozi wa wilaya husika hutuma maombi ya fedha za 
kifuta jasho/machozi kwa Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori. Aidha, 
Afisa kutoka Makao Makuu ya Idara ya Wanyamapori hutembelea eneo husika 
ili kuhakiki uharibifu uliotokea kabla ya kufanya malipo endapo kuna 
haja ya kufanya hivyo. Baada ya taratibu kukamilika fedha za kifuta 
jasho/machozi hutumwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri husika ambapo 
huwapatiwa waathirika au ndugu wa familia iliyoathirika.
Viwango vya malipo ya kifuta jasho/machozi ni kama ifuatavyo:-
Kupoteza maisha (kifo) – shilingi 1,000,000/=
Ulemavu wa kudumu – shilingi 500,000/=
Kujeruhiwa – shilingi 200,000/=
Uharibifu wa mazao (kuanzia ekari 1 – 5): 
Umbali wa kilo mita 0.5 kutoka eneo la hifadhi – Hakuna malipo
Umbali  kuanzia kilo mita 1 – 4 kutoka eneo la hifadhi –  25,000/=
Umbali  kilo mita 4 – 5 kutoka eneo la hifadhi –  75,000/=
Umbali  zaidi ya kilo mita 5 kutoka eneo la hifadhi –  100,000/=
Kifo cha ng’ombe – 50,000/=
Kifo cha kondoo, mbuzi, nguruwe, punda – 50,000/=
Vifo vya wanyama wengine – 10,000/=
3. UENDELEZAJI WANYAMAPORI
Mfuko
 hugharimia shughuli mbalimbali za usimamizi wa wanyamapori ikiwa ni 
pamoja na usimamizi wa maeneo ya jumuiya za hifadhi za wanyamapori 
(WMAs), kutoa elimu ya uhifadhi kwa jamii, usimamizi wa maeneo ya 
ardhoevu na uendelezaji wa miundombinu (nyumba za watumishi, barabara, 
mipaka na viwanja vya ndege) katika mapori ya akiba.
4. UTAFITI, TAKWIMU NA MAFUNZO
Mfuko
 hugharamia mafunzo ya muda mrefu kwa watumishi wa Idara ya Wanyamapori 
wanaosoma katika vyuo vya Mweka na Pasiansi. Pia hugharamia mafunzo ya 
muda mfupi kwa watumishi wa Idara katika vyuo mbalimbali ndani ya nchi. 
Aidha, Mfuko huchangia uendeshaji wa vyuo vilivyo chini ya Idara ambavyo
 ni Pasiansi na Likuyu-Sekamaganga.
Pia Mfuko huchangia gharama za utafiti na kuidadi wanyamapori kupitia taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI).
5. MATUMIZI YA WANYAMAPORI
Mfuko
 hugharamia usimamizi wa matumizi ya wanyamapori ambazo ni: ukusanyaji 
wa maduhuli, usimamizi wa uwindaji wa kitalii na wa wenyeji, utalii wa 
picha, biashara ya wanyamapori hai na mazao yatokanayo na wanyamapori, 
mashamba na bustani za ufugaji wa wanyamapori.
6. MIRADI YA MAENDELEO YA JAMII
Mfuko
 huchangia utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo kwenye jamii 
zinazozunguka maeneo yaliyohifadhiwa. Miradi hiyo ni ile ya maji, afya, 
elimu na miradi ya vikundi vya wajasiriamali. Mfuko huchangia kwenye 
miradi hiyo ili kuwezesha wananchi kuona faida za kuhifadhi wanyamapori.
 
Miradi
 hiyo ni pamoja na: ujenzi wa uzio wa shule ya walemavu- Ilembula 
(Njombe), ujenzi wa vyoo, mabafu na ununuzi wa vitanda- shule ya 
sekondari ya Namanga (Longido), ukarabati wa bwawa katika kijiji cha 
Mwakiloba- Wilaya ya Magu, ujenzi wa zahanati katika kata ya Kwadelo- 
Kondoa, kuchangia ununuzi wa sare na vifaa vya shule kwa ajili ya watoto
 yatima 168 katika Wilaya za Nachingwea, Kilwa, Lindi vijijini na 
Liwale, ujenzi wa madarasa katika shule ya Sekondari ya Luduga- Njombe, 
ununuzi wa mashine ya kusaga ya kikundi cha Enaboishu kijiji cha 
Kitendeni- Wilaya ya Longido na Ujenzi wa bweni katika Shule ya 
Sekondari Wiliam Lukuvi- Iringa.
7. CHANGAMOTO
Katika
 kutekeleza majukumu yake Mfuko unakabiliwa na changamoto mbalimbali 
kubwa ikiwa ni ufinyu wa bajeti ikilinganishwa na mahitaji yaliyopo.
8. MIKAKATI
Katika
 kukabiliana na changamoto hizo Mfuko unaendelea kutafuta vyanzo vipya 
vya mapato zaidi ya biashara ya uwindaji wa kitalii ambao ndicho chanzo 
kikuu cha mapato kwa sasa. Miradi ya maendeleo ya Mfuko imebuniwa ili 
kuiendeleza kwa ajili ya kuongeza mapato ya Mfuko. Miradi hiyo ni Ujenzi
 wa Jengo la Kakakuona, Pori la Akiba Pande, Bustani ya Wanyamapori ya 
Tabora, Bustani ya Wanyamapori ya Ruhila (Songea) na Kambi ya Utalii 
katika Pori la Akiba Selous. Miradi hiyo iko katika hatua mbalimbali za 
kuiendeleza.
9. HITIMISHO
Utekelezaji
 wa majukumu ya Mfuko hauwezi kufanikiwa bila nguvu ya pamoja na 
ushirikiano kutoka kwa wananchi husasan katika kupambana na ujangili. 
Hivyo, wananchi wanapaswa kushiriki kikamilifu katika ulinzi wa 
wanyamapori na mazingira yao kwa faida ya kizazi cha sasa na kizazi 
kijacho cha watanzania.


0 comments:
Post a Comment