Friday, May 15, 2015

Real Madrid na FC Barcelona ndio wanaonufaika zaidi na haki ya matangazo ya televisheni nchini Hispania

Na Shaffih Dauda
KWA wanaofuatilia mpira wa miguu kwa ukaribu zaidi wanafahamu stori kubwa ya mgomo wa chama cha wachezaji Hispania (Players Union), wakipinga muswada uliopelekwa Serikalini na bodi ya ligi, LFP ( ( Liga Nacional de Fútbol Profesional), chombo kinachoendesha soka la Hispania.
Muundo wa soka la Hispania kama wa Bongo vile, Ligi kuu (La Liga) na ligi daraja la kwanza (Segunda division) zipo chini ya Bodi ya Ligi.
LFP na serikali wameleta muswada katika makubaliano ya haki za matangazo ya televisheni wakitaka makubaliano yafanyike kwa pamoja kama ligi kuu England, lengo lao ni kuongeza ufanisi kwa kuzinufaisha timu zote kuliko ilivyo sasa ambapo klabu zinakubaliana zenyewe na makampuni yanayorusha moja kwa moja ‘Laivu’ mechi za ligi kuu na ligi daraja la kwanza.
Kinachotokea Hispania ni kwamba,  FC Barcelona na Real Madrid wana ushawishi na mvuto mkubwa, wanafuatiliwa sana, hivyo makampuni mengi hivi sasa yanavutiwa kuingia mikataba na klabu hizo mbili, matokeo yake nusu ya pesa inayolipwa kwa ajili ya haki za matangazo ya televisheni inachukuliwa na miamba hii ya soka nchini humo.
Madhara yake ni kwamba klabu hizi mbili zimekuwa na msuli mkubwa wa fedha kuliko klabu nyingine na ili kuweza kupunguza pengo lililopo, serikali ambayo inanufaika pia na haki za matangazo ya Telesheni kwasababu wachezaji wanalipa kodi imeona ni bora kubadilisha mfumo.
Mishahara inapoongezeka kwa wachezaji,  kodi nayo inaongezeka, ili kuongeza pato, serikali inaona ni bora kuwepo na makubaliano ya pamoja katika haki za matangazo ya Televishei wakiamini wanaweza kuzisaidia klabu nyingine za chini ili ziweze kupata ‘mzigo’ wa maana na kuweza kulipa mishahara ya maana kwa wachezaji ambao wanalipa kodi serikalini.
Lakini kilichosababisha mgomo unaoendelea hivi sasa ni kutoshirikishwa kwa chama cha soka Hispania kwenye huo mpango unaosimamiwa na serikali ya Hispania na chombo huru kinachoendesha ligi yaani Bodi ya Ligi (LFP).
Chama kimeamua kusimamisha michezo yote mpaka pale watakapokaa meza moja na serikali pamoja na FLP kwa lengo la kutetea maslahi yao kwasababu katika mgao mpya uliokuja unaonesha chama cha soka kina mgao wa asilimia 4 ya jumla ya fedha zote zinazotokana na haki za matangazo ya televisheni na wameona ni kidogo.
 Zaidi chama kinaona kimepunjwa kwenye ule mchakato wa awali na wanaamini kama wangeshirikishwa wangekuwa na hoja za msingi za kuwafanya waweze kupata mzigo wa maana.
Lakini upande wa pili, chama cha wachezaji (Players Union) kimeungana na chama cha soka kupinga muswada huo wakisema kuna baadhi ya vipengele vitakavyoendelea  kuwanyonya wachezaji.
Wanapointi mbili, mosi; pamoja na gawio ambalo baadaye watakuja kupata pamoja kwa maana ya klabu za ligi kuu na daraja la kwanza, bado timu za Segunda division zitapata kiasi kidogo cha fedha ambazo haziwezi kusaidia.
Pili; wale wachezaji wa Ligi kuu (La Liga) wakiangalia vipengele vya pamoja kwenye mgawanyo mpya wa haki za Matangazo, hawaoni nafasi ya klabu za chini kupata hela ya maana na matokeo yake wachezaji wa chini hawatanufaika na mfumo huu mpya.
Pia wachezaji hao wanaocheza ligi kuu wanasema ule mgawanyo mpya utawaathiri wao kwasababu hauongezi pato kwa klabu zao zaidi ya kutengeneza mazingira ya pesa nyingi kwenda serikalini.
Wanaamini kama watakubali mfumo huo itafika mahali klabu zitapunguza mishahara yao kwasababu pato litapungua ikiwa ni matokeo ya utaratibu mpya ambao watu wengi wanaamini ndio suluhusisho la uchumi wa soka la Hispania katika ngazi ya klabu. Kutokana na sababu hizo wameamua kugoma kwenda kujadili muswada huo mpaka pale ambapo baadhi ya vipengele vitakapoangaliwa upya.
Kutokana na suala hili kuna jambo muhimu la kujifunza ukija katika mchakato wa huku kwetu Tanzania. Mkataba wa haki za Matangazo ya Televisheni walioingia Azam TV na bodi ya ligi kuu (TPLB) unakufanya ujifunze kirahisi kuwa kuna rushwa ilitembea, huhitaji kwenda shule ili kufanya uchunguzi kugundau kuwa rushwa ilitembea wakati wa mchakato wa kusainiwa kwa mkataba ule.
Katika hali ya kawaida, haiwezekani kwamba klabu zote zipate gawio sawa kutokana na haki za matangazo ya televisheni (Milioni 100 kutoka Azam TV).  
Huu mgogoro unaondelea Hispania baina ya chama cha soka, chama cha wachezaji, bodi ya ligi na serikali unatufumbua macho sisi tuliopo dunia ya mbali ili walau tuweze kujifunza. Ingawa si kwa kufuata kila kitu kwasababu wenzetu wameendelea sana, lakini ni muhimu kupata maarifa machache ambayo tunaweza kuyatumia katika mazingira ya kwetu kwa lengo la kupata tija katika soka letu.
Cha kwanza, kwa muundo wa bodi ya ligi kuu ya kwetu inayohusisha ligi kuu na ligi daraja la kwanza, timu zote za ligi kuu na ligi daraja la kwanza zinatakiwa kunufaika na haki za matangazo ya Televisheni kwasababu  mkataba unasainiwa kati ya bodi ya ligi na Televisheni (Azam TV) ambayo inaundwa na timu za ligi kuu na ligi daraja la kwanza.
Haiwezekani kila mapato yanayopatikana katika bodi yasizihusu klabu za ligi daraja la kwanza, yaani sawasawa na wewe una watoto wa kuwazaa nyumbani kwako na watoto wa mjomba au Shangazi, unapika chakula, lakini ikifika wakati wa kupakua msosi unawaambia watoto wa Shangazi au mjomba kwamba ‘chakula hiki hakiwahusu’.
Watoto wote wanaishi kwenye familia moja (timu za ligi kuu na daraja la kwanza), ingawa watoto wako wa kuwazaa wanaweza kunufaika zaidi, lakini lazima watoto wengine wanufaike pia kwa kiasi fulani.
Kitu walichotufumbua macho Hispania ni kwamba; mikataba yote wanayoingia Bodi ya ligi kuu, klabu za ligi daraja la kwanza zihusishwe wakati wanakwenda kufanya mazungumzo ya haki za matangazo ya Televisheni kwasababu nao ni sehemu ya wanachama wa bodi.
Lazima zihusishwe kwa maana ya maamuzi ya pamoja katika haki za matangazo. Kwa mfano Azam TV kwa kutotambua wanaweza kutumia fedha nyingi  kuingia mkataba wa ligi kuu na ligi daraja la kwanza, kumbe wao wana haki ya kukubaliana kwa pamoja kwasababu wanafikia makubaliano na bodi ya ligi na sio klabu moja moja. Kama wangekuwa wanakubaliana na timu moja moja, wangeweza kuchagua Simba, Yanga na Azam.
Kwa vile wanakubaliana na bodi ambayo inajumuisha klabu za ligi kuu na ligi daraja la kwanza, Azam TV wao wanatakiwa kuja na fedha ya pamoja, halafu bodi wao ndio wanakaa chini kutengeneza gawio la pesa kwa klabu za ligi kuu na daraja la kwanza.
Kwasababu klabu za ligi kuu mechi zao zinaoneshwa nyingi wanaweza kupata asilimia 90 na klabu za ligi daraja la kwanza zipate asilimia 10 kwa kuwa mechi zao  zinaoneshwa chache.
Kingine cha kujifunza ni nguvu ya wachezaji katika mikataba, kwa mfano chama cha wachezaji cha soka la Hispania kinagoma kucheza kwasababu wanaona vipengele vilivyomo katika mkataba vikisainiwa bila chombo chao kuhusishwa kitawaathiri wao moja kwa moja katika mazingira makuu mawili,
Kwanza ule mkataba ukisainiwa, mapato yao kwa maana ya mishahara na bonasi vitapungua kutokana na klabu kushuka kimapato.
Pili; mfumo huu haujengi mazingira mazuri kwa hawa ambao tunasema hawana kitu (timu za segunda division). Utaratibu mpya hauji kuwafanya wapate zaidi bali unakuja kuwadidimiza. kwahiyo wao kama chama cha wachezaji wameungana na chama cha soka kugoma kwasababu  kwenye huo mkataba hakuna mazingira ya wao kama wahusika wakuu kunufaika.
Ukija kwetu Bongo ukilinganisha na haya yanayofanyika Hispania, kumbe hata hii mikataba wanayoingia bodi ya ligi, wachezaji nao wanatakiwa kuwa na chama chao kinachoweza kuungana kugomea vipengele vya mikataba vinavyowanyonya wao.
Chama cha wachezaji kinatakiwa kuwa na wanasheria, wataalamu ambao wanaingia kwenye vikao na kuwasilisha maslahi ya wachezaji. Haimaanishi  Jonas Mkude kuwa mchezaji wa Simba, basi Simba wana mamlaka yote ya kufanya chochote, lazima kuwepo mipaka, uhusiano wa klabu na mchezaji upo uwanjani kwa kufunga magoli na kucheza dakika 90, lakini linapokuja suala la maslahi pamoja na biashara linaangalia kwa jicho lingine, wachezaji wanatakiwa kuwa na watu wanaowasimamia.
Mchezaji lazima naye apate stahiki yake katika mikataba inayosainiwa, ukiangalia wachezaji wa ulaya kama Cristiano Ronaldo, klabu yake ya Real Madrid ina mkataba na kampuni ya Adidas kwa ajili ya kuwavalisha jezi wachezaji, kwasababu Ronaldo anachezea timu ambayo ina mkataba na Adidas basi analazimika kuvaa jezi ya Adidas, lakini mchezaji halazimishwi kuvaa kiatu cha Adidas kwasababu mguu ni wake mwenyewe.
Ndio maana Ronaldo anavaa kiatu cha Nike kwasababu ana mkataba nao binafsi kama mchezaji. Akiwa katika mazingira ya nje ya klabu anavaa nguo za Nike, akiwa anafanya mkutano na waandishi wa habari unaomuhusu yeye na mambo yake anavaa nguo ya Nike, lakini akiwa anafanya kwa kuiwakilisha klabu, anavaa nguo za klabu ambazo ni Adidas.
Hii maana yake ni kwamba, wachezaji wana nguvu,  wana nafasi kubwa kwa kila kinachofanywa na klabu au chombo chochote kinachosimamia mpira na kuingiza pato kwa kumuhusisha yeye.
Ndio maana wacheza nchini Hispania wanaamua kugoma kwasababu ule mkataba unawaathiri moja kwa moja na wanaona wakiingia mkataba huo mpya mapato yao yatashuka kwasababu klabu badala ya kupata kwa mfano milioni 100 sasa itapata milioni 70.
Kama klabu itashusha kimapato, maana yake itarudi huku chini kukata baadhi ya gharama za uendeshaji ikiwemo kupunguza mishahara kutokana na chanzo mojawapo cha mapato kupungua (haki za matangazo ya Televisheni).
Wachezaji wa Kibongo wajitambue kwa kuangalia wachezaji wa Hispania walivyoanzisha mgomo wakitetea maslahi yao bila kujali kama muswada ule una faida au hapana. Wao wanatumia wataalamu wao ambao wapo kwenye chama chao, wanatetea maslahi yao, wanawaeleza kuwa humu ndani ya mkataba kuna vipengele ambavyo keshokutwa vitawaathiri ninyi moja kwa moja, wao  kama wawakilishi wa chama hawakubaliani na vipengele hivyo na wamewataka wachezaji kutumia nguvu yao  kugoma.
Kibongobongo, tunapoelekea kusaini mikataba mipya, lazima tukubali kutumia wataalamu wenye uelewa wa kujadiliana kuhusu haki za matangazo ya Televisheni ili watetee maslahi ya  klabu pamoja na wachezaji.
Klabu ziwe na chombo chao chenye watu wenye uelewe, ambao wanakwenda kutetea maslahi ya klabu. Pia wawepo viongozi wa klabu wanaotetea maslahi ya wachezaji.
Kilichopo Bongo, ‘Third Part” kwa maana ya makampuni wanapata urahisi kwasababu viongozi wengi wa mpira hawaendi kutetea maslahi ya klabu wala wachezaji, wapo  kwa ajili ya kutetea maslahi yao na ndio maana unakuta madhamini anakuja anasaini mkataba rahisi kwasababu wanaokwenda kufanya mazungumzo ya mkataba hawana taaluma yoyote, wanarubuniwa kirahisi kwa kupewa hela (rushwa)  ili waweze kukubali matakwa ya makampuni ya udhamini na kuridhia kusaini  mikataba ambayo wadau na wataalamu wa soka wanaona ni ‘Bomu’.

Nawatakia siku njema!

0 comments:

 
https://www.sexmutant.com/ https://www.sexindrag.com/ porn movies sex videos hd porno video