Waziri
 wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, akizungumza na 
waandishi wa habari Dar es Salaam jana kuhusu kukamilika kwa awamu ya 
kwanza ya Operesheni ‘Kimbunga’ ya kuwaondoa wahamiaji haramu. Kulia ni 
Kaimu Kamishina wa Uraia na Pasipoti wa Uhamiaji, Victoria Lembeli. 
Picha na Emmanuel Herman 
………..
Dar es Salaam. Waziri wa Mambo 
ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi amewataka Watanzania kuchukua 
hadhari dhidi ya raia wa kigeni wakati huu ambao amani ya dunia ipo 
shakani.
Tamko hilo limekuja wakati kundi
 la kigaidi la Al-Shabaab limevamia jengo kubwa la biashara la Westgate 
huko Nairobi, Kenya na kuua zaidi ya watu 60 huku mamia wakijeruhiwa na 
wengine kadhaa kuendelea kushikiliwa mateka tangu Jumamosi iliyopita.
Hata hivyo, Dk Nchimbi hakugusia
 tukio hilo kwenye maelezo yake lakini aliwataka Watanzania waache tabia
 ya kuwapa hifadhi raia wa kigeni akisema ni hatari kwa usalama wa 
taifa… “Watanzania lazima tuwe makini hasa nyakati hizi ambazo usalama 
wa dunia upo shakani.”
Alisema Serikali kwa upande 
wake, imekuwa ikijitahidi kuweka nchi katika hali ya usalama ikiwa ni 
pamoja na kuendesha operesheni za kuwasaka wahamiaji haramu.
“Hakuna uhalali wa mtu kukaa 
katika nchi nyingine bila kufuata taratibu za sheria,” alisema na 
kuongeza: “Ni lazima vyombo vya usalama kujua nani kaingia na nani 
anaondoka.”
Alisema operesheni inayoendelea 
ya kuwabaini na kuwachukulia hatua wahamiaji haramu inayojulikana kwa 
jina la Kimbunga, waziri huyo alisema imebainika kuwa baadhi ya 
Watanzania wanawahifadhi raia wanaoishi nchini kinyume cha sheria.
Alitoa mfano wa raia wa 
Uingereza ambaye alikuwa akitafutwa na nchi yake kutokana na vitendo vya
 kigaidi lakini akakamatwa akiwa amehifadhiwa na Mtanzania ambaye 
alikwishamfanyia mipango ya kupata vitambulisho kama kile cha mpiga 
kura.
Alisema mkakati wa kuwaondoa 
raia wa kigeni ulianza Julai 26, mwaka huu Rais Jakaya Kikwete alipotoa 
kipindi cha wiki mbili watu wanaoishi nchini kinyume cha taratibu 
kuondoka kwa hiari yao.
“Katika agizo hilo la Mheshimiwa Rais (Jakaya) Kikwete, raia wa kigeni 21,758 waliondoka na kurejea makwao kwa hiari,” alisema.
Dk Nchimbi alisema operesheni ya
 kuwaondoa wale ambao hawakutii amri ya Rais Kikwete ilianza Septemba 6,
 mwaka huu na hadi ilipomalizika wiki hii, watu 12,604 walikuwa wametiwa
 mbaroni.
“Kati ya hao Wanyarwanda ni 
3,448, Warundi 6,125, Waganda 2,496, Wakongo 589, Wasomali 44, Myemeni 
mmoja na Mhindi mmoja,” alisema Dk Nchimbi.
Kwenye
 operesheni hiyo alisema pia waliwakamata watuhumiwa 212 wa unyang’anyi 
pamoja na silaha mbalimbali zipatazo 61, baadhi zikiwa za kivita.
Alisema awamu ya pili ya 
operesheni ya kuwakamata wahamiaji haramu ipo mbioni ingawa alisema 
safari hii, idadi ya watakaounda timu ya uendeshaji wake itapungua.
Waziri
 huyo alisema kuwa wale wote wanaoishi nchini wanaweza kuamua kuondoka, 
kufanya mkakati wa kuomba uraia au kuwa na hati ya kusafiria pamoja na 
kibali cha kuwaruhusu kuishi nchini.
CHANZO: MWANANCHI


0 comments:
Post a Comment