Na Baraka Mpenja
Nyasi za dimba la kumbukumbu ya
hayati Edward Moringe Sokonne jijini Mbeya zitahimili daluga za wanaume wa
jeshi la magereza Wajelajela Tanzania Prisons dhidi ya wapigwa kwata wa Ruvu
Shooting kutoka maeneo ya Pwani ya
Tanzania katika mchezo wa ligi kuu soka Tanzania bara utakaopigwa leo hii.
Prisons wataingia uwanjani wakiwa na
hamasa kubwa baada ya kuwafumua Mgambo JKT kutoka Tanga “waja leo waondoka leo”
bao 1-0 jumatano ya wiki hii jijini humo.
Akizungumza na mtandao huu kutoka
jijini Mbeya Kocha mkuu wa Prisons Jumanne Chale, amesema kikosi chake kipo
shwari na wachezaji wake wamejengeka kisaikolojia kufuatia kupata ushindi adimu
katika uwanja wao wa nyumbani.
“Kiukweli tunahangaika sana kutafuta
ushindi katika uwanja wetu wa nyumbani, tangu tuingie katika ligi msimu huu
tumeshinda mechi tatu tu nyumbani, hakika imetuumiza kwa siku nyingi, lakini
ushindi dhidi ya Mgambo umetujengea imani ya kufanya vizuri leo hii”. Alisema
Chale.
Chale ameongeza kuwa morali ya timu
imekuwa kubwa baada ya wapenzi wa soka jijini humo kuamua kwa moyo mmoja
kuwashangilia kufa na kupona ikiwa ni pamoja na kuwachangia fedha za
kuwahamasisha.
“Sisi si yatima tena, kamati ya
kutusaidia tushinde mechi zote zilizosalia chini ya kamanda wa Polisi mkoani
hapa Diwani Athman Msuya imetupa nguvu sana na kama mambo yatakuwa hivi lazima
tubaki ligi kuu”. Aliongeza Chale.
Kocha huyo ambaye aliwahi kuwanoa
Africa Lyon kabla ya kusaini mkataba na Prisons alisisitiza kuwa hakika msimu
huu umekuwa mgumu sana kwao kutokana na timu nyingi kuwa na wachezaji wazuri
hivyo kusababisha ushindani mkubwa.
Wakati Prisons wakisema maandalizi
yamekamili kwa ajili ya mchezo huo, nao Ruvu shooting waliopo mkoani humo, wamesema
katika mchezo huo wenyeji wao hawatoki.
Kocha mkuu wa klabu hiyo, Charles
Boniface Mkwasa “Master” alisema wanajua
mchezo huo ni muhimu sana kwao kutokana na ukweli kwamba kuna kamati maalumu
iliyoundwa kuwasaidia Prisons wasishuke daraja, lakini bila shaka watachanga
karata zao vizuri na kupata ushindi ugenini.
“Tumetoka kucheza na Polisi moro
jumatano ya wiki hii, tulitoa suluhu nao, tumesafiri mpaka hapa mbeya, lengo
letu ni kufuta matokeo mabaya tuliyoyapa hivi karibuni na kutafuta ushindi kwa
nguvu zote”. Alijigamba Mkwasa.
Mtanange wa Tanzania Prisons dhidi ya
Ruvu Shooting utakuwa wa kukata na shoka kutokana na wenyeji kuhitaji mzigo wa
pointi tatu ili waendelee kujijengea mazingira salama ya kukwepa rungu la
kuporomoka daraja, wakati Shooting wao wanahitaji nafasi nzuri zaidi katika
msimamo wa ligi hiyo.
End…………………..
0 comments:
Post a Comment