Wednesday, April 8, 2015


Na Ezekiel Kamwaga
Wakati nilipokuwa Msemaji na hatimaye Katibu Mkuu wa Klabu ya Simba, hakuna tawi nililokuwanalo karibu kama lile la Mpira na Maendeleo. Kulikuwa na sababu kuu mbili, mosi ilikuwa ni ukaribu wake na ofisi yangu na pili ubunifu iliokuwa nao.

Ukaribu ninaouzungumzia ni ule kwamba mara nyingi walikuwa wakifanya shughuli zao katika eneo la Makao Makuu ya Klabu ya Msimbazi jijini Dar es Salaam. Haikuwa rahisi kupita siku moja ya kazi pasipo kukutana na walau mwanachama mmoja wa tawi hilo.

Ubunifu ninaouzungumzia ni ule wa tawi lile kutengeneza vitu kama kalenda na picha ambazo baadaye waliziuza na kupata fedha za kuendeshea shughuli zao.

Ni katika mazingira hayo ya kazi, ndipo nikakutana na mtu aliyeitwa Mohamed Kingolile maarufu kwa jina la utani la ‘Ngumi Jiwe’ aliyefariki dunia katika ajali ya basi wiki iliyopita mjini Morogoro wakati yeye na wenzake wakiwa njia kwenda mkoani Shinyanga kutazama mechi baina ya Simba na Kagera Sugar. Wanachama sita walifariki katika jail hiyo.

Yeye ndiye aliyekuwa Katibu wa Tawi na kwa namna zaidi ya moja; kiongozi wa tawi hilo.

Viongozi wengi wa Simba, na vilabu vingine hapa nchini, katika ngazi ya matawi wamefariki dunia na sikuwahi kuwaandikia tanzia. Leo, nimewiwa kumuandikia Ngumi Jiwe kwa sababu ya kuwaenzi watu wote wa aina yake waliotangulia mbele ya haki bila kufahamika kitaifa ingawa walikuwa na mchango mkubwa kwenye mchezo wa soka.
Kingolile na wenzake katika kundi hilo, walikuwa wakihakikisha wamefika klabuni kuanzia saa 12 na nusu asubuhi hadi saa mbili asubuhi kwa ajili ya kupiga soga za mchezo wa soka.

Mijadala hii ilikuwa muhimu kwa watu ambao hawakwenda kutazama mechi iliyopita ya Simba au hawana kuelewa kuhusu habari mpya inayoihusu klabu. Kwa wafanyakazi wa mjini ambao wanalazimika kufika mjini kabla ofisi zao hazijafunguliwa, Msimbazi ni ‘kijiwe’ cha kupotezea muda kabla watu hawajaenda kwenye shughuli zao.

Watu wengi hawafahamu lakini kwenye kundi la Mpira na Maendeleo kuna mtu pale anaitwa Chinga kutokana na kwamba anatoka mikoa ya Kusini mwa Tanzania lakini wenzake wanamwita Shafih Dauda. Amepewa jina hilo kwa sababu ya uwezo wake wa kuelezea mchezo.

Yaani, kuna watu wanampa fedha ili aende kuangalia mechi uwanjani ili baada ya mchezo, iwe kesho yake au siku yoyote, aweze kuwaeleza wasiokwenda kuhusu kilichotokea. Kama kuna mchezaji mpya kasajiliwa na Simba na amefanya mazoezi kwa siku moja tu na Chinga akamuona, muulize tu na atakwamba kama mchezaji ni mzuri au mbaya.

Akina Ngumi Jiwe pasipo kuwa na uwezo wa kifedha, walikuwa tayari kusafiri kwa gharama yoyote kwenda popote ambako Simba inacheza. Mara nyingi wakiwasili katika mkoa husika siku ileile ya mechi na kugeuza kurudi Dar es Salaam mara baada ya mechi.

Ngumi Jiwe ni miongoni mwa watu waliokuwa tayari kufanya lolote kuisaidia Simba ipate ushindi. Kuna mambo mengi ya kuitafutia klabu ushindi alikuwa akiyafanya ambayo kwa sababu maalumu sitayataja katika makala hii.
Mara nyingi Kingolile alikuwa anakaa katika kiti cha mbele upande wa pili wa dereva wakati wanaposafiri. Lengo lilikuwa ni kuweza kusikika kwa urahisi wakati anapotaka kutoa taarifa akiwa ndani ya gari lakini pia akiwa pale mbele watu wanaoliona basi wanajua Ngumi Jiwe yupo.

Katika mpira wa Tanzania ambao bado haujafanyiwa mikakati mikubwa ya kutangazwa, mabasi ya washabiki ni sehemu moja ya hamasa zinazotangaza mchezo huu. Hata kama mtu alikuwa hana mpango wa kwenda mpirani, yale mashamsham ya kina Kingolile barabarani huwafanya watu kubadili mawazo na kuja viwanjani.

Siku zote ninaamini kuwa watu kama akina Kingolile ndiyo wanaofanya washabiki wa mpira waendelee kwenda viwanjani hapa nchini wakati katika nchi jirani idadi inapungua kila kukicha.

Niliwahi kwenda kutazama mechi ya Ligi Kuu ya Soka ya Uganda miaka miwili iliyopita katika Uwanja wa Mandela jijini Kampala, na nilisikitika kuona watu chini ya 400 wakiwa wamekwenda kutazama mechi hiyo.

Ukichunguza kwa makini, pamoja na sababu nyingine zinazotajwa ikiwamo nguvu ya Ligi Kuu ya England, utabaini kuwa mojawapo ya sababu ni nchi hiyo kutokuwa tena na akina Kingolile na matawi ya vilabu kama Mpira na Maendeleo, Mpira Pesa, Wekundu wa Terminal, Yanga Bomba na mengine.

Watu wanaofanya mchezo huu uzidi kuvutia, kama akina Kingolile, yule Yamungu wa Morogoro na wengineo, wanapaswa nao kutambulika kama sehemu ya watu wanaopaswa kuheshimiwa. Hawa ni watu ambao maisha yao yote wameyatoa kwa sababu ya mchezo huu.

Sikumbuki kama nimewahi kuzungumza na Ngumi Jiwe kuhusu jambo lingine lolote zaidi ya mchezo wa soka na klabu ya Simba. Leo atakuja na hili na kesho atakuja na lile. Lakini kila siku yeye ni Simba tu na si kingine.

Kwa bahati mbaya sana, watu wa namna hii, kwa sababu hawakuwahi kushika nyadhifa za juu kwenye vilabu hivi vikubwa, wanapokufa huondoka na mambo yao. Kinachouma ni kwamba, watu huwa hatupotezi muda wetu kuwaelewa.

Mimi ni mmoja wa watu waliosikitika baada ya kusikia Kingolile na wenzake wamepigwa mkoani Morogoro baada ya mechi dhidi ya Polisi eti kwa madai ya kuihujumu Simba. Ngumi Jiwe ninayemfahamu mimi asingeweza kuihujumu Simba. Ataihujumu vipi timu ambayo ikifungwa anapata maradhi?

Angeweza vipi kuihujumu timu ambayo alikuwa akipiga ngoma na kucheza kwa dakika zote tisini wakati ikicheza pasipo kujali imefungwa au la? Angewezaje kuihujumu timu ambayo sasa amemwaga damu yake kwayo?
Kama kuna jambo ambalo wana Simba wanatakiwa kulifanya sasa ni kuondoa ile dhana kwamba kuna wanachama ambao hawaitakii mema klabu. Damu hii ya wanachama sita waliokufa kwenye ajali na wengine waliojeruhiwa inatakiwa imwagilie mti wa amani na maelewano.

Mtawala wa zamani wa Ulaya, Attila, alipata kusema miaka mingi iliyopita kwamba “ Si kila mpinzani wako ni adui”. Inawezekana kuna aina fulani ya upinzani ndani ya klabu lakini hali hii haiwezi kufanywa kuwa uadui wa wanachama kupigana wenyewe kwa wenyewe.

Chukulia tu kwamba kwenye nchi yetu kuna CCM, CUF, Chadema na vyama vingine ambavyo japo vinakinzana lakini wanachama wake wanazungumza na kucheka pamoja. Inawezekana pia ndani ya Simba kukawa na Ukawa, Mpira Pesa na makundi mengine. 

Kuna tofauti za kisera na kimtazamo kuhusu mambo fulani lakini Umoja unatakiwa ubaki palepale. Kama anayetakiwa na Simba Ukawa akiwa madarakani isiwe nongwa na anayetakiwa na Mpira Pesa akishinda isiwe nongwa pia kwani wote wanajenga nyumba moja.

Kama ningekuwa kiongozi wa Mpira na Maendeleo leo ningeagiza kwamba itengenezwe bendera kubwa yenye rangi nyekundu na nyeupe ambayo ina picha ya Kingolile itakayokuwa uwanjani kila Simba inapocheza. Hata kama kimwili hayuko nasi, atakuwepo uwanjani kiroho kila wakati klabu inapocheza !

Kama ambavyo Bill Shankly, Bob Paisley na Joe Fagan wanavyoonekana kwenye Uwanja wa Anfield kila Liverpool inapocheza. Ni kwa namna hii pekee ya kuwaenzi watu kama Ngumi Jiwe, ndivyo ambavyo tutawatengeneza wengi wengine. Na soka letu litazidi kupata washabiki.

Ingawa Kingolile ameondoka, ni imani yangu kwamba kile alichofanya kitaendelea kufanywa na wengine wa aina yake. Watu kama Fihi Kambi, Ustaadh Masoud, Abdallah Kazumari, Chinga, Martin Kumalija, Haruna Nazi, Makoye na wengine ambao maisha yao wameyatoa kwa ajili ya klabu ya Simba na mpira wa Tanzania kwa ujumla wake.
Kwa namna yao waliyoamua. 

Mungu awalaze pema peponi marehemu wote waliofariki katika ajali ya Morogoro ya basi la Mpira na Maendeleo.
Mwisho

0 comments:

 
https://www.sexmutant.com/ https://www.sexindrag.com/ porn movies sex videos hd porno video