Na zito Zuberi Kabwe
'Dar inachangia asilimia 80 ya mapato. Kitovu cha Uchumi. Dar inachangia 90% ya ufisadi. Uti wa mgongo wa ufisadi nchini'
Malumbano
 kati ya wananchi wa Mtwara na Serikali kuhusu matumizi bora ya utajiri 
wa nchi yameendelea kwa takribani wiki moja sasa. Baada ya Mkuu wa Mkoa 
wa Mtwara na Waziri wa Nishati na Madini kuwaita Watanzania wa Mtwara 
Wahaini, wapuuzi na watu hatari, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
 naye aliingia kwenye mjadala huo kwa kuonya watu wanaowaunga mkono watu
 wa Mtwara na kuwaita watu wanaotafuta umaarufu wa kisiasa na wanaotaka 
kugawa nchi. Siku moja baada ya hotuba ya Rais, Waziri wa Nishati na 
Madini alifanya mkutano na waandishi wa habari kueleza suala lile lile 
ambalo bosi wake alilielezea usiku wa kuamkia mwaka mpya 2013. Hii ni 
dalili ya Serikali kuweweseka.
Katika
 kauli ya Serikali, ambayo haikuwa na jipya zaidi ya wimbo ule ule wa 
‘kugawa nchi’ ‘umaarufu wa kisiasa’ nk, Serikali ilitaka kuonyesha umma 
kuwa watu wa Mtwara hawana shukurani. Kwamba miaka yote toka Uhuru watu 
wa Mtwara wamekuwa wakilishwa na Pamba, Kahawa, Chai, Tumbaku, Sukari, 
Kidatu nk. Kwamba watu wa Mtwara na Lindi hawakuchangia hata kidogo 
kwenye hazina ya Taifa. Hivyo wao kupigia kelele gesi yao ni uchoyo na 
roho mbaya na kukosa shukurani. Kauli ya Serikali ni kauli ya chombo 
kinachoendelea kukosa ‘legitimacy’ ya kuongoza taifa. Ni kauli ya kukata
 tamaa. Ni kauli hatari sana dhidi ya Watanzania waliojitolea damu 
kulinda uhuru wa nchi yetu.
Moja,
 Serikali katika kauli yake haitaji kabisa kwamba toka Uhuru watu wa 
Mtwara na Lindi wamekuwa wachangiaji wakubwa sana katika uchumi wa Taifa
 kupitia zao la Korosho. Takwimu za Uzalishaji wa Korosho zinaonyesha 
kwamba kuanzia mwaka 1965 mpaka 2011 Korosho imeliingizia Taifa fedha 
kigeni jumla ya dola za Kimarekani 4.58 bilioni ( Cashewnuts Sub-sector 
study 2003, Hali ya Uchumi 2012, Cashewnuts Tanzania Report 2010). 
Katika Mwaka wa Uchumi unaoishia Novemba 2012, Korosho imeliingizia 
Taifa jumla ya dola za Kimarekani 151 milioni. Katika mwaka 2011 zao 
hili liliingiza dola 130 milioni wakati Pamba iliingiza dola 53 milioni 
tu. Licha ya Zao la Korosho kuingiza fedha hizi za kigeni  (sawa ni 
shilingi trilioni 7.2) kwa nchi mikoa ya Lindi na Mtwara ipo miaka 50 
nyuma kimaendeleo kulinganisha na mikoa mingine ya Tanzania. Serikali 
inataka kufuta historia ya mchango wa zao la Korosho kwenye uchumi wa 
nchi yetu kwa sababu ya uroho wa gesi asilia. Kwa nini kauli rasmi ya 
Serikali haijataja Korosho kabisa? Kauli hii ilipitishwa na ngazi zote 
za Serikali? Mawaziri wa Serikali wanaotoka mikoa ya Lindi na Mtwara 
walikubali kauli kama hii itoke dhidi ya wananchi wao wanaoteseka na zao
 la Korosho miaka nenda miaka rudi?
Pili,
 Serikali imesahau kabisa mchango wa watu wa Lindi na Mtwara katika 
ulinzi wa Taifa letu. Moja ya sababu ya mikoa ya Lindi na Mtwara kuwa 
nyuma kimaendeleo ni juhudi za ukombozi wa kusini mwa Afrika. Kambi ya 
wapigania uhuru wa Msumbiji ilikuwa Nachingwea. Kambi ya Frelimo 
iliwekwa kwenye Shamba la Mkonge kilometa 17 tu kutoka mjini Nachingwea 
ambapo ilikuwa makao makuu ya ukombozi wa Msumbiji. Rais Samora Machel, 
Rais Joaqim Chissano na Rais Guebuza waliendesha mapambano kutoka kusini
 mwa Tanzania. Makaburu wa Afrika Kusini na Wareno walikuwa 
wanashambulia nchi yetu na mikoa hii miwili ya Lindi na Mtwara ikawa 
‘buffer zone’. Wakati Dar es Salaam inaendelea kwa kila aina ya 
maendeleo, mikoa ya Lindi na Mtwara ilikuwa inalinda ili wanaoishi Dar 
es Salaam na mikoa mingine waishi wa amani na starehe. Serikali 
inapimaje mchango huu wa mikoa hii? Tunaipima kwa fedha? Uroho wa gesi 
asilia kuzalisha umeme wa kufurahisha walalaheri asilimia 14 nchini ndio
 inaifanya Serikali kusahau kabisa ‘sacrifice’ ya watu wa Mtwara katika 
kulinda uhuru wa Taifa letu?
Tatu,
 Serikali inasema lazima bomba lije Dar es Salaam kwa sababu Dar ndio 
inazalisha asilimia 80 ya Mapato ya Serikali. Kwanza huu ni uwongo. Ni 
aibu Serikali kujitetea kwa uwongo. Dar es Salaam ni kituo tu cha 
kukusanyia mapato ya Serikali. Uzalishaji mkubwa wa nchi yetu wenye 
kuzalisha kodi unafanyika nje ya Dar es Salaam. Walipa kodi wakubwa 
wengi Ofisi zao Kuu zipo Dar es Salaam lakini uzalishaji wao unafanyika 
nje ya Dar es Salaam. Serikali itoe orodha ya walipa kodi wakubwa 100 
tuone uzalishaji halisi wa mapato hayo unafanyika wapi. Hata hivyo 
inawezekana kuwa ikawa kweli Dar es Salaam inakusanya asilimia 80 ya 
mapato ya nchi. Basi na tuseme Dar es Salaam inachangia asilimia 90 ya 
ufisadi wote nchini. Kashfa zote kubwa za Ufisadi zinafanyika Dar es 
Salaam na fedha nyingi za ufisadi zinatumika Dar es Salaam.
Mwisho,
 maandamano ya watu wa Mtwara ni kielelezo tosha kwamba watu wa mikoa ya
 Lindi na Mtwara wamechoshwa na longolongo za Serikali. Wananchi wa 
Mtwara na Lindi wanataka Uwajibikaji wa Serikali kuhusu utajiri wa nchi.
 Mtanzania yeyote mwenye tahadhari ya nchi yetu kutokuwa na laana ya 
rasilimali ataungana mkono na watu wa Lindi na Mtwara kudai maendeleo. 
Nilitoa mfano wa Mgodi wa Golden Pride ambao umemaliza dhahabu yote tani
 76 katika eneo la Lusu wilayani Nzega. Kampuni ya Resolute ya 
Australia iliwekeza dola 370 milioni kuanzia mwaka 1998 (mkataba wao 
ulisainiwa 25th June 1997). Katika kipindi cha uhai wa mgodi, miaka 14, 
 Kampuni hii imeuza dhahabu ya thamani ya dola za kimarekani 3.3 
bilioni. Kabla Serikali haijawaita watu Mtwara wahaini, wapuuzi na watu 
hatari, iwaambie watu Watanzania kodi kiasi gani imekusanywa kutoka 
mgodi huu katika kipindi cha miaka 14. Mpaka mwaka 2008, kwa mujibu wa 
Taarifa ya Kamati ya Bomani, kampuni hii ilikuwa imelipa mrahaba wa dola
 11 milioni na kodi nyingine dola 16 milioni. Serikali itwambie ilipofika Disemba 2012 kodi kiasi imekusanywa kutoka kampuni hii?
Pia
 watu wa Mtwara na Lindi wameona historia ya bomba la Songosongo. Hata 
kodi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (0.3%) ilikuwa inalipwa 
Halmashauri ya Manispaa Ilala na kampuni ya Pan Africa Energy. Ilichukua
 juhudi za mbunge wa Kilwa Kaskazini Murtaza Mangungu kuingilia kati 
ndio kodi ikaanza kulipwa Kilwa ambapo uzalishaji unafanyika. Watu wa 
Mtwara ni werevu, wanajua wafanyalo. Wanataka utajiri wa nchi unufaishe 
nchi kwa kuanzia kule utajiri ulipo. Kuna dhambi gani?
Uwajibikaji
 katika uvunaji wa Rasilimali ya Gesi ndio chanzo cha maandamano ya watu
 wa Mtwara. Serikali isikimbilie kulaumu wanasiasa kwamba ndio 
wamechochea maandamano haya. Haya ni maandamno ya wananchi wakitaka 
Serikali yao iwajibike kwao. Serikali ithubutu kufanya ubabe wa kujenga 
bomba la gesi bila ridhaa ya Wananchi wa Lindi na Mtwara. Wananchi 
wanapohitaji uwajibikaji ni wajibu wa Serikali kuwajibika kwao ni sio 
kuwaita wahaini, wachochezi, watu hatari, wapuuzi. Watu wa Mtwara 
wamechangia maendeleo ya Taifa letu kwa jasho na damu. Serikali ina 
wajibu wa kuwasikiliza, kuwaelimisha na kupata mwafaka. Kauli ya 
Serikali imewatukana watu wa Mtwara na Lindi. Hawatakubali 
kudhalilishwa. Hawatakubali historia yao kufutwa. Hawatakubali waendelee
 kubaki nyuma kimaendeleo. Serikali ifikirie tena.




0 comments:
Post a Comment